Ufugaji wa Bata Mzinga Tanzania

Ufugaji wa bata mzinga Tanzania ni lazima kuhakikisha una chakula cha kutosha kwa sababu ulishaji wake kadri wanavyokua huwa na gharama kubwa zaidi.

Ni muhimu pia kujifunza kwa undani na kufahamu namna ya kutunza vifaranga wa bata mzinga kwa kuwa hufa kwa urahisi sana.

Pia unapaswa kujikita kutafuta soko kwa sababu wanapokuwa ni vigumu kuwatunza kwa muda mrefu kutokana na ukubwa wa gharama ya chakula.

Wafugaji wachache kati ya wengi waliojaribu kuwafuga ndege hawa na kufanikiwa hata kufikia malengo yao ni kutokana na kuzingatia lishe kamili.

Pamoja na hayo, wapo wafugaji ambao walishindwa kutokana na magonjwa pamoja na gharama ya utunzaji.

Chakula Cha Bata Mzinga

Chakula cha bata mzinga hakina tofauti na cha kuku. Vifaranga wanahitaji kupata lishe kamili yenye protini kwa wingi ili waweze kukua vizuri.

Vifaranga kwa siku za awali wanahitaji kiasi cha asilimia 27 ya protini mpaka wanapofikia umri wa wiki sita na baada ya hapo mfugaji anaweza kupunguza hadi kufikia asilimia 18, na kuendelea hivyo hadi wanapokomaa. 

Kutokana na gharama ya kununua chakula kuwa kubwa, unaweza kutumia orodha ifuatayo kwa ajili ya kutengeneza chakula cha bata mzinga wewe mwenyewe.

Mahitaji Ya Chakula Cha Bata Mzinga

  • Mahindi 5kg (yasiyokuwa na dawa)
  • Karanga 5kg
  • Dagaa 5kg
  • Mashudu 10kg
  • Chokaa 5kg (chokaa inayotumika kwa lishe ya mifugo)

Jinsi Ya kutengeneza chakula

Twanga au saga pamoja kiasi cha kulainika kisha walishe vifaranga. Mchanganyiko huu hutegemeana na wingi wa bata mzinga unaowafuga.

Hakikisha kila bata anapata chakula cha kutosha na chenye uwiano ulioelekezwa. Pia waangalie mara kwa mara kuhakikisha wana chakula cha kutosha pia Hifadhi chakula cha ziada kwenye mifuko au debe kisha weka sehemu isiyo na unyevu.

Utagaji wa Bata Mzinga

Bata mzinga huanza kutaga anapofikisha umri wa mwaka mmoja. Ndege hawa wana uwezo wa kutaga kati ya mayai 15 hadi 20 kwa mara ya kwanza na kisha kuhatamia.

Anapoendelea kukua huweza kutaga hadi mayai 30 na Hii ni kulingana na lishe nzuri atakayopatiwa.

Bata mzinga anaweza kuhatamia mayai 17 hadi 20. Mayai hayo huhatamiwa kwa siku 28 na huanza kuanguliwa vifaranga kwa muda wa siku 3, kuanzia siku ya 28 hadi 31.

Baada ya hapo mayai yaliyosalia bila kuanguliwa hutakiwa kutupwa kwa kuwa hayatoanguliwa tena na hayafai kwa matumizi mengine.

Utunzaji wa Vifaranga Vya Bata Mzinga

Baada ya vifaranga kuanguliwa, watenge na mama yao kwa kuwaweka kwenye banda safi lisilopitisha baridi. Unaweza kuwawekea taa ya kandili au ya umeme endapo upo kwenye sehemu unakopatikana.

Banda Zuri La Bata Mzinga

Ni vyema banda liwe limesakafiwa au banda la asili la udongo usiotuhamisha maji. Pia, unaweza kutumia banda lenye mbao au mabanzi kwa chini.

Unaweza pia kutandaza maranda kwenye mabanda. Hakikisha kuta za banda zimefunikwa vizuri ili kuwakinga dhidi ya baridi.

Maji Ya Kunywa Bata Mzinga

Kama ilivyo ndege wengine, bata mzinga pia wanahitaji kupatiwa maji masafi na ya kutosha wakati wote. Wawekee maji katika chombo ambacho hawatamwaga na wanakifikia vizuri.

Hakikisha maji hayamwagiki bandani kwani kwa kufanya hivyo banda litachafuka na kukaribisha magonjwa kwa urahisi. 

Ni vizuri kuwalisha bata mzinga vyakula vingine kama majani. Majani husaidia kuwapatia protini: mfano; kunde, fiwi na aina nyingine za majani jamii ya mikunde huhitajika zaidi kwa kiasi cha 25% hadi 30%.

Magonjwa Ya Bata Mzinga

Bata mzinga hushambuliwa na magonjwa kama taifodi, mafua na kuharisha damu. Wanapougua ni rahisi kuambukiza kuku, bata na ndege wengine wanaofugwa kwa haraka sana.

Pia ndege hawa husumbuliwa na viroboto wanaosababishwa na uchafu wa banda hasa linapokuwa na vumbi.

Chanjo Nzuri Kwa Bata Mzinga

Bata mzinga wanatakiwa kupatiwa chanjo ya ndui (mara moja kila mwaka), kideri (kila baada ya miezi mitatu), gumboro (kwa muda wa wiki tano – ukiwapa jumatatu, basi unawapatia kila jumatatu ya wiki), na vitamini A mara baada ya kuanguliwa.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply