Ufugaji wa Nguruwe Jike Tanzania

Ufugaji wa nguruwe bora wa majike ni muhimu kwani utamuwezesha mfugaji kupata Nguruwe wengi na bora.

Katika ufugaji wa nguruwe Majike wazazi watunzwe vizuri ili kuongeza idadi Ya watoto watakaozaliwa kwa mwaka na kuongeza faida kwa mfugaji.

Utunzaji bora wa nguruwe ni kiini cha idadi ya watoto watakaozaliwa, watakaoishi na Muda watakaochukua kufikia uzito wa kuuza na gharama zitakazotumika.

1. Jinsi ya kuchagua nguruwe bora

Mfugaji anashauriwa kuchagua nguruwe jike anayetegemewa kuwa mzazi kwa kuzingatia sifa zifuatazo

  • Awe amezaliwa na mama anayezaa watoto wengi, mwenye kutoa maziwa mengi na mtunzaji mzuri wa watoto
  • Awe na afya nzuri
  • Awe na kiwele kikubwa chenye chuchu kati ya 10 hadi 14
  • Awe ni Mrefu na mwenye uwiano mzuri kati ya urefu, upana na kimo
  • Awe na umbile la kumuwezesha kubeba mimba na kuzaa kwa urahisi
  • Awe na miguu imara iliyonyooka, kwato imara pamoja na mgongo wenye nguvu na uliopinda kiasi
  • Awe mpole
  • Atokane na wazazi wasiokuwa na historia ya magonjwa au kilema cha kurithi.

2. Jinsi ya kupandisha nguruwe

Katika ufugaji wa nguruwe mara nyingi Nguruwe jike anaanza kuonyesha dalili za joto akiwana umri wa miezi sita hadi saba.

Hata hivyo inashauriwa kutompandisha kipindi hicho ili kuzuia kuzaliwa watoto wenye uzito mdogo, kupata mtatizo wakati wa kuzaa, afya mbaya na kudumaa.

Hivyo basi inapendekezwa nguruwe apandishwe atakapoonyesha dalili za joto kwa mara ya pili au ya tatu.

Kwa kawaida nguruwe huwa tayari kupandishwaakiwa na umri wa miezi  kati ya nane na tisa kutegemea afya na aina ya nguruwe.

3. Jinsi ya kumtambua nguruwe mwenye joto

Katika ufugaji wa nguruwe Mfugaji anashauriwa kuwachunguza nguruwe sio chini ya mara mbili kwa siku hususani asubuhi na jioni wakati wa kuwalisha ili kutambua dalili za joto.

Dalili za nguruwe jike aliye kwenye joto

  • Nguruwe Hupoteza hamu ya kula
  • Nguruwe Hutoa sauti ya kugugumia
  • Huhangaika mara kwa mara
  • Hupandwa na wenzake na hutulia akipandwa au akigandamizwa mgongoni
  • Sehemu ya uke huvimba na huwa nyekundu
  • Hukojoa mara kwa mara na hutoa ute
  • Husimama wima na hutulia akiwa ametanua miguu ya nyuma na mkia ukielekea juu wakati akipandwa na dume.

Dalili hizi sio lazima zionekane zote wakati mmoja hivyo ni jambo la muhimu kuwa mwangalifu.

Ili dalili hizi ziweze kuonekana vizuri, chumba cha majike yanayotarajiwa kupandwa kinatakiwa kiwe karibu na cha dume. Pia Joto kwa nguruwe hudumu kwa muda wa siku mbili hadi tatu.

Mambo ya kuzngatia kwenye kumpandisha nguruwe jike

  • Nguruwe jike apandishwe mara mbili kwa siku hususani asubuhi na jioni.
  • Nguruwe apandishwe masaa 12 hadi 24 anapoonyesha dalili za kusimama akipandwa na dume au akigandamizwa mgongoni Kwa kawaida nguruwe hurudia kuingia kwenye joto kila baada ya siku 21 ikiwa hana mimba.
  • Mfugaji anashauriwa kumchunguza ngurwe jike baada ya kumpandisha Kama ataingia kwenye joto baada ya kupandishwa. Wakati wa kumpandisha inashauriwa nguruwe jike kupelekwa kwenye chumba cha dume ili kuzuia dume kushambuliwa na jike.

Nguruwe ambaye hashiki mimba baada ya kupandishwa mara nyingi inashauriwa mfugaji kumuona Daktari wa mifugo kwa ushauri.

4. Ulishaji wa nguruwe jike

Kabla ya kupandishwa nguruwe jike apewe kilo 2.5 hadi 3 za chakula kwa siku na kupewa maji safi na ya kutosha wakati wote.

5. Jinsi ya kumtunza nguruwe mwenye mimba

Utunzaji bora wa nguruwe mwenye mimba ni muhimu katika ufugaji wa nguruwe ili kupata watoto wenye uzito mkubwa na afya bora.

Pia husaidia nguruwe kuwa na afya bora, kutoa maziwa mengi nakupunguza vifo vya watoto.

Mimba ya nguruwe ni miezi mingapi?

Mimba ya nguruwe ni siku 114 hadi 119 (miezi mitatu,wiki tatu na siku tatu) hadi kuzaa. Kwa kipindi hicho nguruwe anahitaj lishe bora na maji, hewa safi na ya kutosha, mazoezi pamoja na kinga dhidi ya magonjwa. Hivyo, inashauriwa banda liwe na nafasi ya kutosha, na safi muda wote.

6. Chakula Cha nguruwe mwenye mimba

Nguruwe mwenye mimba katika ufugaji wa nguruwe anahitajika kupewa cha kula kinacholeta nguvu na kujenga mwili. Inashauriwa, mwezi wa kwanza wa umri wa mimba apewe kilo 2 hadi 2.5 kwa nguruwe mwenye afya nzuri, akiwa dhaifu apewe kilo 3 kwa majuma matatu.

Pia, baada ya siku 84 za umri wa mimba apewe kilo 2 za chakula kwa siku na kuongeza nusu kilo kila wiki mpaka siku ya tatu kabla ya kuzaa. Siku tatu kabla ya kuzaa, chakula kipunguzwe hadi kufikia kilo 2 kwa siku

Pia wapewe majani kama luseni au chakula chenye nyuzi nyuzi nyingi kama pumba kilo moja kwa siku tatu kabla ya kuzaa ili kuzuia tatizo la kinyesi kuwa kigumu ambacho hushindwa kutoka na kusababisha nguruwe kuzaa kwa shida.

Siku ya kuzaa nguruwe asipewe chakula apewe maji tuu.

7. Jinsi ya kumkinga nguruwe

Nguruwe wenye mimba huathiriwa zaidi na minyoo na magonjwa mengine. Minyoo hupunguza hamu ya kula na hivyo huathiri afya ya nguruwe pamoja na ukuaji wa mimba.

Katika ufugaji wa nguruwe Uzuiaji wa magonjwa na wadudu ni muhumu kwa afya ya nguruwe mwenye mimba. Mfugaji anashauriwa kuwapa nguruwe dawa ya kuzuia minyoo siku 21 hadi 28 kabla ya kuzaa

Kuzuia wadudu, unashauriwa katika ufugaji wa nguruwe kuwaogesha kwa dawa zakuogeshea angalau mara mbili kwa wiki ili kuzuia ukurutu na matatizo mengine ya ngozi.

kwenye sehemu ambazo kuna ndorobo, mfugaji anashauriwa kuwachanja nguruwe. Ni muhimu banda na vifaa vya kulishia na maji viwe safi wakati wote.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

2 Comments
  1. Nashukuru kwa elimu nzuri ya ufugaji wa nguruwe Asante na nategemea nitaendelea kujifunza zaidi.

Leave a reply