Ufugaji wa Funza Tanzania

Ufugaji wa Funza ni mzuri sana kwa Tanzania pia funza ni aina ya wadudu ambao wanapatikana kwenye mbolea ya samadi inayotokana na mifugo kama vile ng’ombe, mbuzi, kondoo na nguruwe.

Sehemu Ambapo Funza Wanazalishwa

Funza wanaweza kuzalishwa kutokana na kinyesi cha wanyama kama vile ng’ombe, mbuzi, kondoo, na nguruwe kwa kuchanganywa na tope chujio linalotokana na mtambo wa biogas.

Sehemu ya kuzalishia Funza

Funza hupendelea sehemu isiyokuwa na joto kali wala baridi sana, hivyo ni muhimu kuandaa sehemu yenye kivuli kwa ajili ya uzalishaji wa funza.

Sehemu ya uzalishaji wa funza, inaweza kutumika kwa muda wa miezi sita.

Muda Unaochukua Kufuga Funza

Funza huchukua muda wa siku 3 kufaa kulishia kuku, tangu mbegu yake kupandikizwa kwenye sehemu ya uzalishaji.

Jinsi Ya Kuzalisha Funza

  1. Andaa sehemu yenye kivuli
  2. Hakikisha udongo hauna magadi. Endapo uko sehemu ambayo udongo una magadi, unaweza kuchukua udongo kutoka sehemu nyingine na kuutanguliza chini kabla ya mbolea
  3. Tandaza udongo huo kiasi cha hatua ishirini
  4. Mwaga tope chujio kutoka katika mtambo wa biogas juu ya udongo ulioandaa kiasi cha kufunika
  5. Weka mbolea uliyoandaa ya ng’ombe na mbuzi juu ya tope chujio (unaweza kutumia mbolea ya ng’ombe pekee)
  6. Weka mbegu ya funza kisha funika kwa kutumia nyasi au majani mengine kuweka joto la wastani
  7. Nyeshea maji kiasi cha kulowana kila siku ili kuweka unyevu unyevu
  8. Funika na baada ya siku tatu, utakuwa tayari kuruhusu kuku kujilisha

Faida za Funza Kwa Kuku

Kutokana na ulishaji wa kuku kwa kutumia funza, wameweza kubaini kuwa kuku wanaongeza uzito kwa haraka na kwa kiasi kikubwa, tofauti na ulishaji wa kawaida.

Muda wa Kuku Kulishwa Funza

Kwa kawaida kuku hulishwa pumba asubuhi mpaka saa saba mchana, muda ambao kuku hao huwa wameshamaliza kutaga.

Baada ya hapo kuku hufunguliwa katika eneo lao la wazi ambalo kunakuwa na matuta ambayo funza wamezalishwa, na kufunguliwa tuta moja baada ya jingine.

Kuku huweza kuwa huru kujilisha kwa kutumia funza hadi jioni, na baada ya hapo kurudi katika mabanda yao bila kulishwa aina nyingine yoyote ya chakula.

Kuku mia mbili (200) wanaweza kulishwa kwa kutumia matuta mawili hadi matatu yenye ukubwa wa mita 20 kwa siku.

Madhara Ya Funza Kwa Kuku

Wagunduzi wa njia hii mpya ya ulishaji kuku wa kienyeji wanasema kuwa, kwa kipindi cha miaka mitatu ambayo wamekuwa wakilisha kuku kwa kutumia funza, hakuna madhara yoyote yaliyoyojitokeza.

Pia wamegundua kinga ya magonjwa imeongezeka kwa kuwa kuna baadhi ya magonjwa ambayo yalikuwa yakiwashambulia kuku hapo kabla, lakini kwa kipindi cha miaka miwili hawajapata tatizo lolote.

Mafanikio Ya Ufugaji wa Funza

Mafanikio ni makubwa, moja wapo ni kupungua kwa gharama za utunzaji kwa upande wa chakula.

Pia ongezeko la kipato kinachotokana na ongezeko la bei kulingana na uzito wa kuku, ambao inaaminika unatokana na aina hiyo mpya ya ulishaji wa kuku kutokana na funza.

Funza Pia ni Chakula cha Samaki

Ulishaji wa kuku kwa kutumia funza ni upande mmoja, lakini upande wa pili hutumika pia kulisha samaki kwenye mabwawa.

Tofauti na ilivyo kwa kuku, funza kwa ajili ya kulisha samaki, huachwa kwa muda mrefu zaidi takribani wiki mbili, ili wawe wakubwa.

Kama ilivyo kwa kuku, imebainika pia kuwa samaki wanapolishwa funza ukuaji na uzito huongezeka kwa haraka, ikiwa ni pamoja na kupunguza gharama za kulisha pia.

Mbolea Baada Ya Kuzalisha Funza

Hakuna madhara yoyote yanayotokana na mbolea iliyotumika kuzalishia funza.

Mbolea iliyotumika kwa ajili ya kuzalisha funza inafaa kabisa kuendelea kutumika shambani na kwenye bustani za mboga kama kawaida.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

1 Comment
  1. Mbegu ya hao funza inapatikanaje ni hawa waliopo kwenye udongo pia Naomba kuelimishwa zaidi.

Leave a reply