Jinsi Ya Kuongea Mbele za Watu

Kuzungumza mbele ya watu kunaweza kuwa ni tatizo ikiwa hujiamini au hujajiandaa vyema Hata hivyo, mazoezi na mtazamo chanya vinaweza kukusaidia kuwa mzungumzaji bora mbele ya watu.

1. Jitahidi Kujiandaa na Kufanya Mazoezi

Watu wengi wamekuwa wakikumbwa na hofu, wasiwasi na hata kutokwa na jasho sana wanapokuwa wanazungumza mbele za watu.

Hii inatokana na kuwa na uzoefu mdogo unaoletwa na kutofanya mazoezi ya kutosha ya kuzungumza mbele ya watu.

Jitahidi kufanya mazoezi ya kuzungumza mbele za watu kwa kutumia njia zifuatazo:

  • Zungumza mbele ya familia au marafi zako mara kwa mara kwa ujasiri.
  • Unaweza kusimama mbele ya kioo chumbani na kufanya mazoezi ya kuzungumzia jambo fulani.
  • Toa michango katika warsha, mikutano na makongamano mbalimbali.
  • Sikiliza na tazama wazungumzaji waliobobea.

Ni dhahiri kuwa ukizingatia haya ndani ya muda mfupi utaweza kuboresha kiwango chako cha kuzungumza mbele ya watu.

2. Jitahidi Kuelewa Hadhira Yako

Kuelewa hadhira yako ni jambo muhimu litakalokuwezesha kufahamu mambo mbalimbali kama vile lugha, mahitaji, mifano na hata maudhui yatakayowasilishwa.

Mambo ya kuzingatia:

  • Jinsia
  • Umri
  • Elimu
  • Imani
  • Hali ya uchumi.

Mambo haya ni muhimu kwani yatakuwezesha kutengeneza hotuba au mazungumzo yanayowalenga wahusika zaidi.

Kwa mfano unapozungumza na wanawake ni vyema ukagusa zaidi mambo yanayowahusu. Pia unapozungumza na watu wa imani au mtazamo fulani ni vyema ukazungumza kwa namna ambayo haitaathiri imani au msimamo wao.

Ni muhimu sana kuifahamu hadhira yako vyema.

3. Jitahidi Kupangilia Utakachozungumza

Ufanisi katika kuzungumza mbele za watu unahitaji kujiandaa na kupangailia vyema vile utakayoyazungumza.

Epuka fikra za mimi nimezoea kazi hii au nalifahamu sana swala hili. Jizoeze kutengeneza mpangilio mzuri wa hotuba au mada utakayoizungumzia.

Pia kumbuka kuandaa mada yako kwa njia ambayo inavutia wasikilizaji na unayoweza kuifuata.

4. Pokea mrejesho na uufanyie kazi

Kipimo cha ubora wako kipo na kinatokana na wasikilizaji au watazamaji wako. Hivyo ni muhimu kupokea mrejesho kutoka kwa hadhira yako na kuufanyia kazi.

Ikiwa wasikilizaji au watazamaji wako watatoa mrejesho kama vile kusema unazungumza haraka sana au kwa sauti ya chini sana, basi jitahidi kuyafanyia kazi.

Kwa kufanya hivi utarekebisha mapungufu yaliyojitokeza na wakati mwingine hayatatokea tena; hivyo utakuwa bora zaidi.

5. Jitahidi Kuwa Mcheshi

Ni vyema kama mtu unayezungumza mbele ya watu utajifunza kuwa mcheshi, kutumia simulizi na lugha vyema.

Epeka kuwachosha wasikilizaji; wafanye wacheke na kufurahi; wasimulie jambo linaloendana na mada japo kwa ufupi ili wasichoshwe na mada yako na kuacha kukusikiliza.

Pia zingatia lugha unayoitumia; hakikisha lugha unayoitumia inakupa uhuru wewe na wasililizaji wako; pia hakikisha unaimudu vyema lugha husika.

6. Jitahidi Usisome Pekee

Watu wengine husoma tu badala ya kuzungumza mbele za watu. Haimaanishi kuwa ikiwa umeandika mada yako basi ndiyo ukaisome kama gazeti mbele ya watu.

Jitahidi kuzungumza zaidi, tena ukitazama hadhira yako; tumia kile ulichoandika kama mwongozo pekee.

Kumbuka, ukisoma badala ya kuzungumza utawafanya wasikilizaji kuchoshwa na kile unachokiwasilisha mbele yao.

7. Jitahidi Kutumia Sauti na Mikono Yako Vyema

Kutokana na kukosa uzoefu pamoja na maandalizi duni watu wengi hujikuta wakipoteza sauti au kushindwa kutumia viungo vya mwili vyema kama vile mikono na mikao ya uso (Facial impresions).

Kuzungumza mbele ya watu kunahitaji matumizi mazuri ya sauti pamoja na viungo kama vile mikono, kwani si jambo jema kusimama au kukaa kama roboti bila hata kujigusa wakati unazungumza mbele ya watu.

Hivyo ni muhimu kuzingatia mambo haya ili uweze kujenga uwezo wa kuzungumza mbele ya watu.

8. Jitahidi Kuteka Usikivu Mwanzoni

Kuna usema usemi usemao “Nyota njema huonekana asubuhi”; ni dhahiri kuwa ukianza kuzungumza mbele ya watu vibaya ndivyo itakavyokuwa kwa mchakato mzima.

Jitahidi kuteka usikivu wa hadhira yako mwanzoni ili wavutiwe kukuzikiliza na kukutazama muda wote unapozungumza.

9. Jitahidi Kutumia Vifaa vya Sauti na Picha Vyema

Kuna wakati mwingine utahitajika kutumia vifaa kama vile vipazasauti au vifaa onyeshi kama vile projekta. Hakikisha unavimudu na umeviandaa vyema kabla ya kuvitumia katika kuzungumza kwako.

Mambo ya kukumbuka:

  • Tazama kama kuna uhitaji wa kifaa husika na je, unaweza kukitumia kwa uhuru? Kwa mfano hakuna haja ya kutumia kipazasauti wakati una sauti ya kutosha na unazungumza na watu wachache tu kama vile 20.
  • Hakikisha kifaa kinafanya kazi vyema na kinafaa kwa hadhira yako.
  • Zingatia watu wenye mahitaji maalumu kama vile viziwi; vipofu, n.k

Kwa kufanya hivi utaweza kujenga uwezo wako wa kimaandalizi katika swala zima la kuzungumza mbele ya watu.

10. Jitahidi Kushirikisha Hadhira

Haimaanishi kuwa, kwa kuwa watu wamekaa ili kukusikiliza basi haihitajiki kuwashirikisha au kusikiliza hoja na mawazo yao.

Hii ni njia bora itakayokuwezesha kuifahamu na kuimudu vyema hadhira yako.

Njia za kushirikisha hadhira:

  • Uliza maswali pia ruhusu kuulizwa maswali
  • Washirikishe katika majadiliano
  • Pokea mapendekezo na maoni yao

Kwa kufanya hivi utavutia zaidi hadhira yako; pia utaweza kupata mambo kadha wa kadha kutoka kwa hadhira yako ambayo yatakuwezesha kuboresha uwezo wako zaidi.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply