Faida za Kuweka Akiba Kwenye Maisha

Kuweka akiba ni kanuni mojawapo ya matumizi mazuri ya pesa. Hata hivyo kutokana na watu wengi kutokuwa na matumizi mazuri ya pesa, bado wengi wanashindwa kuweka akiba.

Baadhi ya watu hufikiri kuwa ili uweze kuweka akiba ni lazima uwe na pesa nyingi, lakini ukweli ni kuwa kuweka akiba ni maamuzi tu na siyo kuwa na pesa nyingi.

1. Akiba inasaidia Kupata Uhuru wa Kifedha

Uhuru wa kifedha ni zaidi ya kuwa na pesa, uhuru wa kifedha ni kuwa mtu ambaye unatakiwa kuwa maishani na kuweza kufanya au kupata kile unachokihitaji maishani.

Hata hivyo pesa ni muhimu sana kwenye swala la uhuru wa kifedha, ingawa pesa hizi zinatakiwa ziambatane na fikra sahihi.

Kwa njia ya kujiwekea akiba utaweza kujijengea msingi mzuri wa kifedha ambao ukiambatanishwa na fikra sahihi utakuletea uhuru wa kifedha.

2. Akiba inasaidia Kuwa na Matumizi Mazuri

Kama nilivyoeleza hapo mwanzo kuwa kuweka akiba siyo kuwa na pesa nyingi bali ni maamuzi na mipango stahiki pekee.

Hivyo kuweka akiba kutakufaidisha kwa kukuwezesha kutumia pesa vyema. Ikiwa unapata elfu kumi kwa siku, itakubidi uitumie vizuri ili uweze kutenga fedha ya akiba.

Kama huweki akiba huna haja ya kutumia pesa vyema kwani hakuna sehemu ya akiba inayotakiwa kutengwa.

3. Akiba inasaidia Kujiaandaa na Dharura

Watu wengi huingia kwenye madeni au kupata uhitaji mkubwa wa pesa mara wapatwapo na dharura. Hivyo kwa kuweka akiba utapata faida ya kukuepushia mahangaiko wakati wa dharura kama vile maradhi, msiba, majanga.

4. Akiba inasaidia Kuweza Kufanya Manunuzi Makubwa

Kuna manunuzi au miradi ambayo inahitaji pesa nyingi ili kuitekeleza. Maswala kama vile ujenzi wa nyumba, ununuzi wa kiwanja, kununua gari, n.k. ni baadhi ya mambo yanayohitaji fedha nyingi.

Hivyo, kwa kuwa na akiba utaweza kutekeleza mambo haya kwa urahisi zaidi kuliko ungeyafanya bila akiba.

5. Akiba inasaidia Kuweza Kumudu Wanaokutegemea

Ikiwa kuna watu wanaokutegemea kama vile wazazi, ndugu au watoto; ni vyema kuweka akiba ili uweze kuwa na fedha ya kukidhi mahitaji yao mara wapatwapo na uhitaji.

Kutokuweka akiba kutakufanya uhangaike huku na huko ukitafuta fedha za kukidhi mahitaji ya wategemezi wako kama vile chakula, matibabu au hata ada za shule.

6. Akiba inasaidia Kuwa na Utulivu wa Akili

Unapokuwa huna akiba yoyote huwezi kuwa na utulivu wa akili. Kila wakati unahofu na wasiwasi juu ya maisha yako, unajiuliza likitokea tatizo itakuaje? Au hitaji fulani linalokuja hivi karibuni litakuwaje? n.k.

Unapokuwa na fungu fulani la akiba huna haja ya kuwa na wasiwasi kwani unajua hata ukikosa fedha akiba yako itakusaidia.

7. Akiba inasaidia Kukuwezesha Kuandaa Kesho Vyema

Maandalizi ya kesho yanafanywa leo na Kuweka akiba maana yake unajiandaa kwa mahitaji ya kifedha ya baadaye yaani kesho. Mtu asiyeweka akiba mara nyingi hafikiri kuhusu kesho wala hana malengo kwa ajili ya baadaye yake.

Ili kujenga baadaye au kesho njema, ni muhimu pia kuimarisha msingi wako wa kiuchumi kwa njia ya kuweka akiba.

8. Akiba inasaidia Kuwahi Fursa

Ni mara ngapi umekuwa ukisema au ukisikia kauli kama vile “Ningekuwa na pesa ningenunua hiki kitu”, “Ningekuwa na pesa ningejiunga kwenye hii huduma” au “Ningekuwa na pesa ningejiunga na huu mradi”.

Hili linadhihirisha kuwa watu hukosa fursa mbalimbali kutokana na kukosa akiba ya fedha. Unapokuwa na akiba ya fedha ni rahisi kuwahi fursa mpya au bidhaa zenye manufaa mara zinapopatikana.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply