Ufugaji wa Kuku wa Kienyeji Tanzania na Ujenzi wa Banda

Ufugaji wa Kuku Utegemea sana Ujenzi wa mabanda imara ya kuku kwasababu ni miongoni mwa mambo ya msingi kabisa katika ufugaji wa kuku iwe ufugaji wa kuku wa asili au hata ufugaji wa kuku wa kienyeji.

Hata hivyo si kila mtindo wa ujenzi unafaa, kwahiyo ujenzi huo ni lazima uzingatie mahitaji halisi ili ufugaji huo uweze kutoa matokeo bora yanayotarajiwa na mfugaji.

Mambo muhimu katika ufugaji wa kuku na ujenzi wa banda la kuku

  • Liingize hewa safi wakati wote
  • Liwe kavu daima.
  • Liwe nafasi ya kutosha.
  • Liwe la gharama nafuu lakini la kudumu.
  • Lizuie kuingia wanyama na wadudu hatari kwa kuku.
  • Liwe na nafasi ya kuweka vyombo vya chakula na maji.
  • Lizuie upepo wakati wa baridi kali.

Hewa na mwanga katika banda la kuku

Hewa ni muhimu kwa kila kiumbe, hivyo banda la kuku ni lazima liingize hewa safi na kutoa ile chafu na liweze kuingiza mwanga wa kutosha.

1. Kwa kifupi ni kwamba madirisha ya banda ni lazima yawe makubwa na ya kutosha ili yaingize hewa safi na kutoa ile chafu.

2. Ni vema madirisha haya yawe juu kiasi cha meta moja (1) kutoka chini ili hewa ipite juu ya vichwa vya kuku.

3. Hewa safi siyo upepo, hivyo jaribu kuzuia upepo mkali kuingia ndani ya banda la kuku ili kuepusha kuku kuugua ugonjwa wa mafua na niumonia na pia vifaranga vinaweza kufa kwa ugonjwa wa baridi.

Jenga Banda lako kwa kukinga upepo unakotokea na kupanda miti kuzunguka banda hilo la kuku ili kupunguza kasi ya upepo na kuweka kivuli dhidi ya jua kali na joto.

Ukavu na usafi wa ndani ya banda la kuku

Kwa vile kuku si ndege wa majini kama bata ni jambo la busara kuhakikisha kuwa mahali wanapoishi hapana unyevunyevu.

1. Banda la kuku lijengwe mahali palipoinuka ili kuzuia maji ya mvua yasiingie.

2. Wajengee kuku uchaga wa kulalia kwa kuweka viguzo vyenye urefu wa meta moja na kutandika miti juu yake ili usiku walale hapo, kuliko kuwalaza ardhini au sakafuni.

3. Ukavu wa banda ni muhimu sana hasa kwa vifaranga na kuku wanaotaga. Ndani ya banda lenye unyevu mayai huchafuka sana na hata wakati mwingine huoza kwa urahisi na jitihada zako zitakuwa ni bure.

4. Sakafu ya banda ni vizuri ikawa ya zege lakini kutokana na uhaba wa fedha sakafu inaweza kutengenezwa kwa mabanzi au udongo mgumu na au mchanga ambao utafunikwa kwa mabaki ya taka za mpunga na yale ya mbao.

5. Ili kuepuka unyevunyevu ni vyema eneo/mahali pla kujenga banda pawe pameinuka na penye kupitisha hewa ya kutosha.

6. Paa la banda liwe madhubuti ili kuzuia maji ya mvua kuingia hasa wakati wa masika. Sakafu ya banda iwe juu zaidi ya usawa wa nje.

Paa linaweza kuezekwa kwa mabaki ya vipande vya bati , madebe na kama ikishindikana tumia nyasi zinazofaa kwa ajili ya kuezeka nyumba katika eneo hilo.

Nafasi ya kufanyia kazi katika banda la kuku

Banda la kuku lisiwe na nguzo au mbao nyingi sana ndani kiasi cha kumfanya mhudumiaji wa kuku ashindwe kufanya kazi zake.

Hali hiyo itamfanya apoteze muda mwingi katika kuzizunguka nguzo hizo, hasa wakati wa kuokota mayai au kufanya usafi.

Vifaa vya ufugaji wa kuku

Unapotaka kujenga banda la ufugaji wa kuku kwanza kabisa tayarisha vifaa vinavyotakiwa. Vitu kama miti au nyasi, nyavu au fito, misumari au kamba ni muhimu kuviandaa mapema. Pili ni lazima uwe na plani/ramani kamili ya banda hilo.

Ujenzi rahisi wa banda la kuku

Kuku wafugwao hatimaye ni lazima wafidie gharama za Ujenzi wa mabanda na chakula. Gharama zikiwa kubwa sana huenda ukaifanya shughuli ya ufugaji wa kuku usiwe na faida hata kidogo hali hiyo itamfanya mfugaji aone ufugaji hauna maana yoyote kwake.

Lakini ukijenga banda lako kwa kutumia vifaa vinavyopatikana kwa urahisi utaongeza faida zaidi kwakuwa umepunguza gharama za uendeshaji wa mradi.

Vipimo vya banda la kuku

Banda la kuku linatakiwa liwe na Meta 15 hadi meta 22 za eneo yaani Meta 3 hadi 4.5 za upana kwa meta 5 za urefu. Banda hili linaweza kutunza kuku 100 wakubwa kwa wakati mmoja.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

5 Comments
  1. Asante sana kwa maelekezo haya ya kina juu ya ufugaji wa kuku wa kienyeji

  2. Nalikuwa nawaza kuanzisha mradi wa ufugaji wa kuku haswa wa kienyeji Asante elimu hii nazani itanisaidia sana.

  3. Mwenyezi Mungu akubariki sana nami pia nilikuwa nawaza kuanzisha mradi wa ufugaji wa kuku naamini kwa maelekezo haya nitafanikiwa.

Leave a Reply to Lenald Minja Cancel reply