Ufugaji wa Bata Tanzania

Ufugaji wa Bata kwa Tanzania ni maarufu sana na wafugaji wengi wadogo wa bata hapa nchini hufuga bata machotara ambao pia wapo wa aina mbalimbali.

Matumizi makubwa ya bata hawa ni kwa ajili ya kupata nyama, japokuwa huweza kutumika kwa ajili ya kupata mayai na pia kwa ajili ya mapambo nyumbani.

Aina maarufu ya bata wa nyama ambao pia hufugwa kwa wingi hata kibiashara ni Pekin na asili ya bata hawa ni China na utawatambua kwa rangi ambayo ni nyeupe.

Pekin hukua haraka, wana maumbo marefu, vidali vilivyojaa na ngozi zao ni rangi ya njano.

Vichwa na miguu ya bata hawa mekundu iliyochanganyika na njano pia madume ya Pekin huwa na wastani wa kilo 4.5 na majike kilo 4 wakiwa hai

Banda La Kufugia Bata

Paa la banda laweza kuwa la nyasi, makuti, vigae au bati mradi mvua, joto, na baridi kali visiruhusiwe kuwepo ndani.

Kuta za banda la bata zinaweza kujengwa kwa kutumia miti, udongo, mbao, matofali au mabati. Sakafu inaweza kuwa ya saruji, zege au udongo na kuwekewa malalio ya mbao au kwa kutumia maranda.

Sakafu ya nyavu za chuma au fito kama kichanja chaweza kutumika ikinyanyuliwa nusu futi (sentimita 15) kutoka ardhini.

Kwa ujumla banda linatakiwa kuwa kavu na mwanga wa kutosha, lenye kuruhusu mzunguko wa hewa vizuri. Kipimo kiwe ukubwa wa kuweka bata wakubwa watatu katika mita moja ya mraba au wadogo wanaokuwa 6 wenye umri wa wiki 4 katika eneo la ukubwa huohuo.

Jinsi Ya Kuzalisha Bata

  1. Majike ya bata yachaguliwe kutoka kwenye majike mama yenye uwezo wa kutaga mayai mengi, kuatamia vizuri na kutotoa vifaranga vingi (15 hadi 20).
  2. Madume yawe na uwezo wa kupanda yakiwa na umri wa miezi 6 na majike nayo huanza kutaga yakiwa katika umri huohuo.
  3. Inashauriwa madume na majike ya ukoo mmoja katika upandishaji ili kuondoa kurithishwa kwa sifa mbaya katika kizazi kijacho kwa mfano, uwezo mdogo katika utagaji, uanguaji wa mayai, ukuaji hafifu, kushambuliwa kirahisi na magonjwa nakadhalika.
  4. Dume moja la bata lina uwezo wa kupanda/kurutubisha majike 4 hadi 6 na inashauriwa dume na majike wakae pamoja kipindi cha mwezi mmoja au zaidi kabla ya majike kutaga ili mayai yapate muda wa kutosha wa kurutubishwa kabla ya kutagwa.
  5. Majike yana uwezo wa kutaga, kuatamia na kuangua vifaranga 15 hadi 20, uatamiaji huchukua siku 28. Bata aina ya Muscovy kutoka Amerika ya Kusini wao huatamia kwa muda wa siku 35.
  6. Kuku pia anaweza kuatamia na kuangua mayai ya bata ili hakikisha awe na mayai machache maana mayai ya bata ni makubwa kuliko ya kuku (yasizidi 8).
  7. Kwa kuwa kuku hana tabia ya kuoga mara kwa mara kama bata, hivyo inapasa mfugaji kuyawekea unyevunyevu kila siku ili kuboresha joto na unyevunyevu unaohitajika katika uatamiaji.
  8. Waweza kupata vifaranga vya bata na kuku kwa kuanza kumuatamisha kuku mayai ya bata kwa muda wa siku saba, kisha inapofika siku ya nane unamwongezea mayai ya kuku ambapo inapofika siku ya 38 vifaranga vya bata na kuku vitaanguliwa.

Chakula Cha Bata

  1. Kwa upande wa lishe, mahitaji muhimu kilishe huwa sawa kwa wote, awe bata, kuku au hata bata mzinga wanaotumika kwa ajili ya kutaga mayai kwa ajili ya kutotolewa pamoja na madume yao.
  2. Mahitaji ya vifaranga wa bata na vya kuku wa mayai pia hufanana, kwa hiyo vifaranga wa bata wapewe Chick au Duck mash katika wiki 3 za mwanzo na Growers mash kuanzia wiki ya nne mpaka umri wa kuanza kutaga. Chakula cha aina hiyo kinaweza kutengenezwa kwenye viwanda vya mifugo au maduka ya pembejeo za mifugo kama Farmers Centre, Farmbase na kupitia matawi na wakala wao wote mikoani.
  3. Mimea ya kijani, na ya jamii ya mikunde pia chakula bora cha ziada kwa bata wa umri wote ambayo huwapatia vitamini, protini na madini kwa ajili ya kulinda mwili. Majani yanaweza kufidia asilimia 40 ya chakula.
  4. Bata hasa vifaranga hupenda kula chakula chenye hali ya unyevunyevu au majimaji.
  5. Bata wakubwa wana uwezo wa kula punje za nafaka kama kunde au mbegu za mafuta ambavyo huwapatia nguvu, joto na kujenga miili yao.
  6. Punje za nafaka zinaweza kupondwapondwa na kuwa chenga ambazo bata wanaokuwa wanaweza kula kutokana na ukubwa wa midomo yao.

Mambo Ya Kuzingatia Kwenye Ufugaji wa Bata

  1. Katika uleaji wa vifaranga vya bata, hakikisha joto katika wiki ya kwanza linakuwa nyuzijoto 32.2oC hadi 35.5oC. wiki ya pili 26.7oC hadi 29.3oC na katika wiki ya tatu na nne linakuwa 23.9 oC hadi 26.7oC.
  2. Vifaranga vya bata visiogelee kwenye maji wala kunyeshewa mvua ili kuwalinda kutokana na kuathiriwa na baridi (hadi wakifikisha umri wa wiki sita).
  3. Bata hujisugua chini ya mkia na mgongoni ili kulifanya tezi lake litoe mafuta ya kujing’arisha baada ya kuoga.
  4. Idadi ya bata inayofungiwa ndani haiwi kubwa kama ya kuku kwa sababu watu wengi hupenda zaidi ladha ya nyama na mayai ya kuku kuliko bata.
  5. Hata hivyo bata ana uwezo wa kutaga mayai mengi na makubwa kuliko kuku.
  6. Pia anakuwa haraka, ana uwezo wa kula chakula hata kile ambacho hakifai kwa mwanadamu na viumbe wengine bila kuudhuru mwili wake ambao ni sugu.
  7. Wakati wa ukame kuku hana uwezo wa kushindana nao, lakini kuwepo kwa majani mengi mabichi bata hustawi zaidi.
  8. Bata ana uwezo mkubwa zaidi wa kujilinda dhidi ya wanyama na wadudu adui wake na hustamili magonjwa ya aina mbalimbali mathalani Mdondo, Gumboro hata ndui. Ugonjwa pekee unaoshambulia zaidi bata ni homa ya matumbo (typhoid) ambapo dawa ya kunywa ya aina ya Fluban (Enrofloxaxin) imethibitika kudhibiti ugonjwa huu.
  9. Bata pia hushambuliwa na wadudu na wadudu (parasites) mbalimbali ambao hupatikana ndani na nje ya mwili wake kwa mfano wa nje ya mwili ni viroboto, utitiri, chawa, viroboto na ukurutu. Vilevile ndani ya mwili ni kama minyoo ya kwenye utumbo na maini. Dawa ya aina ya Ivermectin ya kunywa imeonyesha uwezo mkubwa katika kudhibiti wadudu wote wanaodhuru bata ndani na nje ya mwili kwa mkupuo.
Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply