Jinsi Ya Kufahamu Bidhaa Feki Kwenye Biashara

Mara nyingi tunanunua vitu na bidhaa mbalimbali Tanzania bila kuzifahamu au kuzichunguza vyema Hili limepelekea watu wengi kununua bidhaa zisizofaa kwao au zenye madhara kwenye afya zao.

Kutokana na ukosefu wa elimu pamoja na kuishi kwa mazoea, watu wengi hawajui wala hawachunguzi vyema bidhaa wanazozinunua ili kuhakikisha ubora wake.

Madhara ya kutumia bidhaa Fake au bandia:

  • Matatizo ya kiafya kama vile saratani na ulemavu.
  • Upotevu wa fedha.
  • Ajali (Milipuko au shoti ya umeme).
  • Huathiri uchumi.

Ni wazi kuwa yapo madhara mengi yatokanayo na matumizi ya bidhaa feki. Hivyo ni vyema ukafahamu njia za kubaini bidhaa hizi.

1. Bidhaa Fake Huwa na Matangazo Yasiyo Ya Kawaida

Wahenga walisema “Chema chajiuza kibaya chajitembeza”; ni vyema ukawa makini na bidhaa zenye punguzo kubwa la bei kuliko kawaida, kwani mara nyingi bei hupungua sana kutokana na ubora duni.

Pia ni vyema ukaepuka kuvutiwa na maneno ya kibiashara kama vile “Oringinal” Colection”, “King size”, “Royal”, “genuine,” “real,”, “authentic”, “Mpya” au “Kali”.

Kumbuka simaanishi usinunue bidhaa yenye punguzo au maneno haya bali yasiwe ndiyo yanatawala au kutumiwa kama mbinu ya mauzo.

2. Jitahidi Fahamu Bidhaa Yako

Ni vyema ukaichunguza na kuifahamu bidhaa ambayo unainunua au kuitumia mara kwa mara. Hili litakuwezesha kubaini bidhaa ambayo ni Fake au bandia kwa urahisi zaidi.

Chunguza na bainisha vitu vya msingi ambavyo ni lazima viwepo kwenye bidhaa husika. Hivyo kabla ya kununua bidhaa hakikisha inafanana na ile uliyoizoea.

kama hujawahi kuinunua unaweza kumwomba mtu anayeifahamu vyema akusaidie kuikagua.

3. Jitahidi Kukagua Vifungashio Kwa Makini

Kubaini bidhaa Fake au bandia kunahitaji utulivu, chukua muda kukagua vifungashio vya bidhaa husika kwa makini.

Hili litakuwezesha kubaini kukosekana kwa taarifa muhimu kama vile jina la mtengenezaji, mahali pa utengenezaji, tarehe ya kuzalishwa na ya mwisho wa matumizi pamoja na taarifa nyingine muhimu.

Bidhaa iliyokosa taarifa muhimu inaweza kuwa bandia au yenye ubora duni.

4. Jitahidi Kuhakikisha Kila Kilichotakiwa Kuwepo Kipo

Mara nyingi unaweza kununua kifaa au bidhaa yenye kitu zaidi ya kimoja Kwa mfano, ikiwa unanunua simu au kamera hakikisha kama huwa inauzwa pamoja na vifaa kama vile betri, chaja, memory card na waya wa USB vipo vyote tena kwenye hali nzuri.

Mara nyingi bidhaa feki hukosa badhi ya vifaa muhimu ambavyo kwa kawaida huwepo kwenye vifaa au bidhaa halisi.

5. Jitahidi Kuuliza Kuhusu Warranty

Warranty ni mkataba maalumu baina ya mnunuzi na mtengenezaji wa bidhaa husika. Warranty hukuwezesha kutengenezewa au kubadilishiwa bidhaa husika ikiwa itapata matatizo ndani ya muda fulani.

Bidhaa bandia au feki kamwe huwa hazitoi Warranty na zikitoa basi ni Fake pia. Hivyo ni vyema ukatazama kama bidhaa husika (Hasa vifaa vya kielektroniki) zina Warranty ya uhakika.

6. Jitahidi Kutembelea Tovuti Ya Mzalishaji

Hivi sasa karibu kila kampuni imejitahidi kufungua tovuti kwa ajili ya kuwafikia wateja wake kwa urahisi zaidi. Pia kampuni nyingi zimekuwa zikijitahidi kuwawezesha wateja wake kubaini bidhaa feki.

Wakati mwingine, baadhi ya bidhaa huwekwa namba ambazo unaweza kuziingiza kwenye tovuti yao na kuona kama bidhaa ni bandia au laa. Hivyo, unaweza pia kutumia njia hii ili kubaini na kuepuka bidhaa Fake.

7. Jitahidi Kununua Kutoka Kwa Wakala Aliyeidhinishwa

Ili kurahisisha na kuhakikisha ubora wa huduma, kampuni nyingi zimekuwa zikisajili mawakala kwenye maeneo mbalimbali.

Unaponunua bidhaa kutoka kwa wakala aliyeidhinishwa, ni rahisi zaidi kupata bidhaa halisi; pia upatapo tatizo utapata msaada kwa urahisi zaidi.

Kwa mfano, ikiwa unataka kununua simu ya Nokia au Sumsung, basi tafuta wakala aliyeidhinishwa na Nokia au Sumsung katika eneo lako.

8. Jitahidi Kuepuka Bidhaa Copy

Hivi leo unaweza kuona simu inayoitwa NOKLA, lakini ukiitazama kila kitu kinafanana na simu ya NOKIA N97.

Kwanini kama watengenezaji wa simu hii wanalengo zuri wasibuni muundo wao wenyewe? Ni dhahiri kuwa wanataka kuwadanganya na kuwachanganya wanunuzi huko kubadili jina na kuiita NOKLA ni mbinu tu ya kukwepa mkono wa sheria.

Ni wazi kuwa bidhaa hizi ni feki, hivyo yakupasa kuziepuka.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply