Aina za Wateja Kwenye Biashara Tanzania

Mteja ni mtu muhimu sana katika biashara yoyote na Lengo la kuanzisha biashara ni kupata wateja watakaonunua bidhaa au  huduma yako.

1. Wateja wapya wa biashara

Hawa ni wateja ambao huja kwenye biashara yako kwa mara ya kwanza, mnaweza kuwa mnafahamiana nje ya biashara, lakini hamjawahi kuhudumiana kwenye biashara.

Mteja huyu huja kwa lengo la kupata huduma pamoja na  kuifahamu biashara husika ili kuona sababu itakayomfanya awe mteja wa biashara hiyo.

Wewe kama mfanyabiashara, hutakiwi kufanya kosa kwa aina hii ya mteja; hakikisha mteja huyu anaifahamu biashara yako vyema na anapata sababu za kutosha za kuanza kuwa mteja wako wa kudumu.

Unaweza kufanya haya yafuatayo kwa mteja huyu:

  • Mpe maelezo kuhusu bidhaa au huduma unazotoa katika biashara yako.
  • Mpe ofa ya ukaribisho.
  • Onyesha sura na lugha nzuri itakayo mfanya aone ujio wake mpya umethaminiwa sana.
  • Ikiwa inawezekana au atahitaji, mpe mawasiliano ya biashara yako pamoja na muda wa utoaji wa huduma.
  • Ikiwa mteja huyu amehama kutoka kwenye biashara nyingine, basi dodosa ni sababu gani zimemfanya ahame. Mara nyingi wateja waliohama husema wao wenyewe kuwa kule walikokuwa walipata changamoto kadha wa kadha hivyo sasa wameamua kuwa wateja wako. Mf. Utasikia mteja akisema “Kule kwenye lile duka fulani wanajisikia sana.”, “Yule muuzaji anauza vitu ghali sana.” n.k. Yachukue haya kama somo la kuboresha huduma yako.

2. Wateja wanaofuata punguzo kwenye biashara

Hii ni aina nyingine ya wateja ambao huja kwenye biashara yako wakiwa katika safari yao ya kutafuta punguzo la bei kwenye huduma au bidhaa wanayoitafuta.

Mara nyingi wateja hawa wanaweza kutekwa na punguzo dogo sana ambalo hata wewe mwenyewe usingedhani kama linaweza kumshawishi mteja kununua huduma au bidhaa yako.

Jambo muhimu hapa inabidi ujue kucheza na bei za bidhaa vizuri, ni bora ukose hata shilingi hamsini au miamoja kwenye faida yako lakini uwapate wateja wa aina hii.

Kwa mfano kuna mteja anaweza kuacha kununua gesi kwenye duka inapouzwa shilingi 20,000 na kwenda kununua wanapouza 19,850 au 19,900. Hivyo, ni muhimu kuwaelewa wateja hawa ili uwapate na ukuze biashara yako.

3. Wateja wa kudumu kwenye biashara

Hawa ni wateja ambao uko nao kila mara, hawa ndio wateja wakuu uliowazoea na waliokuzoea wewe. Hawa ni wateja muhimu ambao wanapaswa kuthaminiwa na kuhudumiwa vyema. 

Mara nyingi wateja hawa wanakuamini na wanaamini huduma na bidhaa ile unayoitoa. 

Tabia kuu za wateja wa kudumu:

  • Wateja hawa hawahamishwi kirahisi, hata kunapokuwa na mterereko wa huduma au bei wengi wao huvumilia.
  • Hupenda kutoa ushauri na mapendekezo kuhusu biashara na huduma kwa kuwa hujihisi kuwa nao ni sehemu ya biashara husika.
  • Mara nyingi huwa mabalozi wema wa biashara husika.
  • Hupenda kuacha pesa zao  kwako na kukopa.

Hivyo basi, wewe kama mjasiriamali hakikisha unaongeza thamani ya huduma kwa wateja hawa ili kujenga msingi imara wa wateja kwa ajili ya  biashara yako. 

4. Wateja mabalozi wa biashara

Ingawa wateja watiifu au wakudumu wanaweza kuwa mabalozi wa biashara yako; sifa hii hujidhihirisha zaidi kwa wateja wale ambao hasa sifa yao kuu ni ubalozi.

Wateja ambao ni mabalozi wanaweza wasiwe ni wateja wa mara kwa mara, lakini wakawa mabalozi wazuri au wabaya wa ile huduma au bidhaa unayouza.

Wateja hawa hupenda kuwashirikisha watu wengine sifa za biashara yako ikiwa ni nzuri au ni mbaya. Wateja hawa huleta marafiki, majirani au hata wanafamilia wao kwenye biashara yako ikiwa wameridhishwa na huduma unayotoa.

Vivyo hivyo, ikiwa wateja hawa hawakuhudumiwa vizuri, wataeneza sifa mbaya ya huduma au bidhaa unazouza.

Hivyo, ni muhimu kuwabaini wateja hawa na kuhakikisha tabia yao ya ubalozi inabeba mbegu au sifa njema kutoka kwenye biashara yako.

Mambo unayoweza kufanya ili kuhimiza wateja kuwa mabalozi wa biashara yako:

  • Toa huduma nzuri ambayo mteja hataisahau au kuona aibu kuitaja kwa mtu mwingine.
  • Toa ofa na punguzo.
  • Mshukuru mteja pale anapokuletea mteja mpya.
  • Tumia lugha nzuri itakayo kufanya uwe mfano.

Kumbuka! Inawezekana kumfanya kila mteja awe balozi mwema wa biashara yako.

5. Wateja watafiti kwenye biashara

Hii ni aina ya wateja ambao hufanya manunuzi baada ya kupata taarifa za kina kuhusu bidhaa au huduma ile wanayoitaka. Hebu tutazame mfano huu:

(Mteja A na Muuzaji A)

Mteja A: “Habari, kuna losheni ya kuondoa chunusi?”

Muuzaji A: “Ipo ya Aloe Vera shilingi elfu tano, nikupe ngapi?”

(Mteja A na Muuzaji B)

Mteja A: “Habari, kuna losheni ya kuondoa chunusi?”

Muuzaji B: “Ndio ipo, unataka ya wanaume au ya wanawake?”

Mteja A: “Ya wanawake”

Muuzaji B: “Ipo ya Aloe Vera  ile OG, hii inaondoa chunusi na haichubui ngozi kabisa, tena nitakushauri jinsi ya kuichanganya ili ikubali zaidi ngozi yako.”

Mteja A: “Unauzaje?”

Muuzaji B: “Moja ni shilingi elfu tano, ila ninaweza kukupunguzia kidogo….ukinunua nyingi pia nitakupunguzia zaidi.”

Kwa kutazama hayo mazungumzo hapo juu unafikiri mteja A atanunua losheni kwa muuzaji A au B? Ni wazi kuwa atanunua kwa muuzaji B kwa sababu anajua kunadi bidhaa yake vyema kwa kuhakikisha mteja anapata maelezo ya kutosha ya bidhaa na bei.

Fahamu vyema huduma na bidhaa unazouza, haifai mteja kuja kwako na kukuuliza kuhusu huduma au bidhaa zako  ukashindwa kumpa maelezo ya kuridhisha. Kumbuka kuwa wateja watafiti wanataka kupata maelezo ya kina kabla hawajafanya manunuzi.

6. Wateja wapitaji kwenye biashara

Hawa ni wateja ambao huja kwenye biashara yako mara moja tu, na si rahisi kuja tena mara nyingine au karibuni.

Mara nyingi wateja wa aina hii huwa ni wasafiri au watu walioletwa kwenye eneo lako la biashara kutokana na tukio fulani kama vile msiba au sherehe.

Ingawa wateja hawa ni wapitaji, unapaswa kuwahudumia vyema kwani hujui kesho itakuwaje. Ili kuwapata wateja hawa ni vizuri kujenga jina jema katika eneo husika ili mteja mgeni afikapo katika eneo unalofanyia biashara akubaini wewe kwanza kabla ya kumbaini mfanyabiashara mwingine.

7. Wateja walalamikaji kwenye biashara

Hii ni aina ya wateja ambao wanapenda kulalamika na kulaumu sana. Si rahisi kuwaridhisha wateja hawa kwani wao kila kitu kwao ni tatizo. Hata hivyo, pamoja na tabia yao hii, bado utaendelea kuwaona wakija kila mara.

Ukimpunguzia bei atasema ni mbinu ya kumvuta umuibie, ukimweleza ubora wa bidhaa atakuambia unamrubuni ili anunue, ukimwambia bei za vitu zimepanda atakuambia unamdanganya…n.k.

Wateja hawa kamwe huwezi kuwaridhisha kwani kila mara huona kuwa mfanyabiashara si mwaminifu au anapata faida kubwa sana kwa ujanja ujanja.

Kwa kuwa wateja hawa hupenda kuongea sana, ni muhimu ukaangalia jinsi ya kutumia hekima kuwajibu na kuwahudumia ili wasije wakaeneza sifa mbaya kwa wateja wengine.

8. Wateja wasiokuwa na mpango wa manunuzi

Je umewahi kununua kitu sokoni au dukani ambacho hakikuwa kwenye mpango wako wa manunuzi kwa kuwa tu umekiona au mtu mwingine amekushawishi kukinunua? Au umewahi kusikia mtu akisema nimenunua hiki kitu kwa sababu nimekuta kinauzwa bei nzuri nikaona nisikiache?

Ikiwa jibu ni ndio, wewe au huyo mtu mwingine wote mlikuwa wateja wasiokuwa na mpango wa manunuzi. Wateja hawa hufanya manunuzi ambayo hawakuyapanga awali; mara nyingi hufanya manunuzi kutokana na tamaa ya macho au ushawishi wa marafiki au muuzaji.

Ikiwa wewe ni mfanyabiashara mwenye ushawishi na unayejua kunadi bidhaa zako vyema, ni rahisi sana kuwapata wateja wa aina hii kwani utaweza kuwashawishi wateja ambao hawakuwa na malengo ya kununua bidhaa zako wazinunue. 

9. Wateja wanaotafuta ubora wa bidhaa

Kutokana na hali ya ugumu wa maisha, wateja wa aina hii ni wachache sana. Wateja wanaotafuta ubora ni aina ya wateja ambao wao hawaoni shida kutumia gharama kubwa kutafuta bidhaa yenye ubora wanaouhitaji.

Wateja hawa hawatishiwi na bei wala hawapendi kuomba punguzo, wanachozingatia ni ubora wa bidhaa au huduma wanayoitaka.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

11 Comments
  1. Ninafanya kazi za kutoa semina kwa wafanya biashara nimeandaa mafunzo mnaweza kushirikia nasi?

  2. Asante sana nimejifunza kitu kutokana na hizi aina za wateja

  3. Ahsante sana Kwa ukaribisho mzuri

  4. Asante sana, Nimepata darasa zuri endelea kutoa elimu hii kwa wafanyabiashara wengi Tanzania ili wawe na ufanisi mzuri katika biashara zao

  5. Asante sana kwa elimu nzuri

  6. Asante sana nimejifunza kitu pia kama una uzoefu na biashara ya karasha tafadhali nisaidie.

  7. Asante sana. sina muda mrefu kuifahamu hii website, lakini kwa nilivyoipekua na kusoma mambo kadhaa tu, nimegundua mko kipekee sana.

    Nilijaribu kutafuta muda mrefu website au blog yenye maelezo mchanganyiko kuhusu business mbalimbali,hatimaye wauzaji.com ndio mmetia fora. Keep it up

Leave a Reply to Lenald Minja Cancel reply