Kilimo Cha Ufuta Tanzania

Kilimo cha ufuta kwa Tanzania ni zao ambalo hulimwa kwa ajili ya chakula na biashara pia mbegu za zao hili huwa na wastani wa mafuta kiasi cha asilimia 45.

Jinsi Ya Kuchagua Mbegu za Ufuta

Chagua aina ya mbegu inayotoa mazao mengi na bora, inayovumilia mashambulizi ya magonjwa na wadudu, inayokomaa mapema na kutoa mafuta mengi.

Chagua mbegu inayokomaa kwa pamoja ili kurahisisha uvunaji na pia kuepuka upotevu wa zao shambani pia aina nyeupe ya mbegu za ufuta hupendelewa zaidi kuliko aina nyeusi. 

Jinsi Ya Kuweka Mbolea Kwenye Ufuta

Ufuta unahitaji rutuba ya kutosha ili kutoa mazao bora. Katika kudumisha rutuba ya udongo, tumia kilimo cha mzunguko wa mazao au weka mbolea za asili pale inapobidi.

Jinsi Ya Kufanya Palizi Kwenye Ufuta

Dhibiti magugu kwa kupalilia ili kuruhusu ufuta kutumia vizuri unyevu na virutubishi. Magugu mengine huwa ni maficho ya wadudu waharibifu wa zao la ufuta.

Magonjwa na Wadudu wa Kilimo Cha Ufuta

Ufuta hushambuliwa na magonjwa na wadudu mbalimbali ambao huweza kusababisha upungufu na ubora wa mazao.

Hivyo kagua shamba mara kwa mara hasa kwenye maua na mapodo ili kuona dalili za mashambulizi. Endapo kuna dalili zamashambulizi, chukua tahadhari mapema kabla ya uharibifu mkubwa haujatokea.

Jinsi Ya Kukagua Shamba La Ufuta

Kagua shamba kuona kama ufuta umekomaa pia ufuta hukomaa, kati ya miezi mitatu na minne tangu kupanda kutegemea aina.

Aina ya ufuta usiokuwa na matawi hukomaa mapema kuliko ile yenye matawi ni muhimu kuwahi kuvuna ili kuepuka ufuta kupukutikia shambani. 

Dalili za Kukomaa Kwa Ufuta Shambani

Kwa kawaida majani hubadilika rangi kutoka kijani na kuwa ya manjano na hatimaye kudondoka pia mashina hubadilika rangi kutoka kijani na kuwa ya kahawia. 

Vifaa vya Kuvunia Ufuta

  • Kamba
  • Siko
  • Panga

Vifaa vya Kukaushia ufuta

  • Sehemu ya kukaushia yenye Sakafu ya saruji
  • Maturubai
  • Sakafu safi

Vifaa vya Kusafirishia Ufuta

  • Mikokoteni
  • Matela ya matrekta
  • Magari 

Jinsi Ya Kuvuna Ufuta Shambani

Vuna ufuta mapema kabla mapodo kukomaa sana na kuanza kupasuka na kuachia punje. Mapodo ya ufuta yaliyokomaa sana yakiguswa au kutikiswa na upepo hupasuka na kuachia mbegu, hali inayosababisha upotevu mkubwa.

Mbegu za ufuta ni ndogo na zikidondoka chini ni vigumu kuziokota. Vilevile mbegu zilizodondoka ni vigumu kuzitenganisha na uchafu.

Uvunaji wa ufuta huhusisha ukataji wa mimea yenye mapodo kwa kutumia vyombo vya mkono kama panga kwa kukata mashina.

Kwa aina za ufuta zenye mapodo yanayopasuka, uvunaji ufanyike wakati mimea bado ni kijani ili kuepuka upotevu wa mbegu.

Aidha uvunaji ufanyike wakati hakuna upepo wala jua kali.

Baada ya kukata mashina yafunge katika mizigo midogo na kuweka katika vyombo vya kusafirisha kama vile mikokoteni, matela au magari hadi sehemu ya kukaushia.

Panga mizigo midogo kwa kusimamisha katika malundo madogo yasiyozidi mizigo minane kwenye sehemu safi za kukaushia.

Jinsi Ya Kukausha Ufuta

Mapodo ya ufuta hukaushwa yakiwa yamefungwa katika vitita. Vitita huwekwa kwa kuegeshwa kwenye fremu ya kukaushia kwa muda wa wiki mbili hadi tatu kutegemea hali ya hewa.

Fremu hii huwekwa juu ya turubai au sakafu ili kuzuia upotevu wa punje kutokana na kupasuka kwa mapodo.

Jinsi Ya Kupuputisha Ufuta

Upuraji hufanyika kwenye turubai, mkeka au kwenye sakafu safi.

Vitita hupigwa taratibu kwa kutumia mti au hutikiswa vikiwa vimegeuzwa vichwa chini ili kuruhusu punje za ufuta kudondoka kwenye sakafu safi au turubai.

Jinsi Ya Kupembua Ufuta

Kupepeta na kupembua hufanywa ili kuondoa takataka kama vile mawe, vipande vya mapodo,vijiti na vumbi.

Njia bora ya kupepeta na kupembua ni kwa kutumia mikono.

Ufuta huwekwa kwenye vyombo kama vile ungo kwa kiasi cha kilo mbili hadi tatu kisha ufuta hurushwa hewani kwa kasi ndogo na takataka nyepesi huchukuliwa na upepo na zile nzito huondolewa kwa mikono. 

Jinsi Ya Kufungasha Ufuta

Mbegu za ufuta zilizo safi huwekwa kwenye vifungashio kama vile magunia madogo ya aina ya juti ya ujazo wa kilo 50.

Fungasha mbegu za ufuta kwenye magunia yenye uzito usiozidi kilo 50. Kabla ya kufungasha hakikisha mbegu zimekauka hadi kufikia unyevu wa asilimia 10.

Jinsi Ya Kuhifadhi Ufuta

  • Panga magunia ya ufuta juu ya chaga.
  • Panga kwa kupishanisha ili kuruhusu mzunguko wa hewa kati ya magunia.

Jinsi Ya Kusindika Mbegu za Ufuta

Ufuta husindikwa kupata bidhaa ya mafuta ambayo hutumika katika mapishi mbalimbali na mafuta hukamuliwa kwa kutumia njia za asili na kwa kutumia mashine.

Njia za asili zina ufanisi mdogo ukilinganisha na zile za kukamua kwa mashine, hivyo ni vyema kutumia mashine.

Kuna mashine za aina mbili zinazotumika kukamua mafuta; mashine za mkono na zile zinazoendeshwa kwa injini au mota ya umeme.

Mashine za mikono zinazotumika zaidi hapa nchini ni za aina ya daraja (Bridge press) na Ram.

Jinsi Ya Kukamua Kwa Mashine Ya Daraja

Mashine ya daraja ni moja ya mashine za kisasa zinazoweza kukamua mafuta ya ufuta na mashine hizi huendeshwa kwa mikono na zina uwezo wa kukamua mafuta kwa asilimia 68 hadi 72.

mashine hizi zinaweza kukamua kilo 25 za ufuta kwa saa moja na ili kupata ufanisi mzuri wa mashine hii ni muhimu ufuta uwe na unyevu wa kati ya asilimia 11 na 13.

iwapo unyevu utakuwa chini ya kiwango hicho inashauriwa kunyunyizi maji kwenye ufuta kabla ya kukamua.

Vifaa Vya Kukamulia Mafuta Ya Ufuta

  • Mashine ya daraja
  • Sufuria na Vifungashio
  • Mifuko midogo ya nguo au viroba vyenye upana wa sentimita 20 na urefu wa sentimita 20.
  • Chombo cha kukinga mafuta.
  • Chujio safi
  • Lebo
  • Lakiri Malighafi
  • Mbegu za ufuta safi
  • Maji safi

Ukamuaji wa Mafuta Ya Alizeti

  1. Nyunyuzia maji kidogo kwenye ufuta ili kuongeza unyevu kufikia asilimia 11 hadi 13. Mafuta hutoka vizuri kwenye kiwango hicho cha unyevu. Jaza ufuta kwenye vifuko vya nguo au viroba
  2. Vipange vifuko hivyo kwenye silinda na kuanza kuzungusha mhimili hadi mafuta yaanze kutoka kupitia matundu ya silinda.
  3. Acha kwa muda mafuta yaendelee kutoka kisha endelea kuzungusha mhimili hadi mafuta yaishe. Mhimili ukiacha kuzunguka ni dalili kuwa mafuta yamekwisha.
  4. Kusanya mafuta, chuja na fungasha kwenye chupa safi zilizochemshwa. Hakikisha chupa ni kavu na zina mifuniko.
  5. Weka lebo na lakiri
  6. Hifadhi mahali pakavu na pasipo na mwanga mkali. 
Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply