Utangulizi wa Kilimo Bora Cha Viazi Vitamu Tanzania

Viazi vitamu ni moja kati ya mazao makuu ya mizizi Tanzania. Kutokana na uwezo wake wa kuvumilia ukame pia zao hili ni moja kati ya mazao ya kinga ya njaa.

Hapa Tanzania zao la viazi vitamu hulimwa zaidi katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Dodoma, Morogoro, Kagera, Arusha na Ruvuma.

Kuna aina mbalimbali za viazi vitamu zikiwemo Ukerewe, Kakamega, Karoti C, Mavuno, Pananzala na Polista.

Zao hili la viazi vitamu hustawi maeneo mengi hapa Tanzania na hukubali vizuri zaidi katika maeneo ya tambarare yenye udongo tifutifu ambao unaruhusu maji kupenya kirahisi.

Udongo mfinyazi na wenye kokoto nyingi haufai kwa ajili ya kilimo hiki kwani huzuia mizizi kupenya na kupanuka.

Kabla ya kuanza rasmi kilimo cha viazi vitamu mkulima anapaswa kuhakikisha shamba linatayarishwa vizuri kwa kufyeka vichaka na kung’oa visiki. Vilevile, majani yanatakiwa kufunikwa wakati wa kutengeneza matuta ili kuiongezea udongo rutuba.

Wataalamu wa kilimo wanashauri kupanda viazi vitamu kwa kutumia mashina yenye urefu wa sentimita 30 kwa matokeo mazuri zaidi. Inashauriwa kutumia sehemu ya juu ya shina kuongeza mavuno.

Mashina yanatakiwa kupandwa katika umbali wa sentimita 25 hadi 30 kutoka mmea hadi mmea na sentimita 60 hadi 75 kutoka tuta hadi tuta. Viazi pia vinaweza kupandwa kwa kutumia viazi vyenye afya na vyenye uzito wa gramu 20 mpaka 30.

Mkulima wa kilimo cha viazi vitamu anatakiwa kupalilia shamba la viazi vitamu miezi miwili ya mwanzo ili kuwezesha mmea kutambaa vizuri. Baada ya muda huo, viazi vitamu huweza kufunika ardhi na hivyo huzuia uotaji wa magugu.

Wadudu kama vile kipepeo, mbawa kavu, fukusi na minyoo fundo ni baadhi ya changamoto za kilimo cha viazi vitamu.

Viazi vitamu pia hushambuliwa na magonjwa mbalimbali yatokanayo na virusi. Magonjwa haya pamoja na uwepo wa wadudu yanaweza kudhibitiwa kwa usafi, kubadilisha mazao pamoja na kuzingatia udhibiti sango.

Kilimo cha viazi vitamu huchukua muda mfupi tu kukomaa, hivyo mkulima anaweza kupata faida mapema. Mara nyingi viazi vitamu huwa tayari kuvunwa kuanzia miezi mitatu hadi minne tangu kupandwa kulingana na hali ya hewa.

Viazi vitamu huvunwa kidogo kidogo kwa kutumia mikono, vijiti, jembe au rato. Mkulima anatakiwa kuhakikisha viazi haviachwi ardhini kwa muda mrefu bila kuvunwa kwani vitakomaa kupita kiasi na kuharibu ubora wake.

Uvunaji wa viazi vitamu unapaswa kufanywa kwa uangalifu mkubwa ili kuhakikisha viazi vitamu havikatwi wala kuchubuliwa wakati wa zoezi hili.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply