
Kilimo cha miti Tanzania kimeendelea kuja kwa kasi hapa nchini Licha ya kwamba uwekezaji katika aina hii ya kilimo huchukua muda mrefu kuona faida yake na inaelezwa kuwa utajiri wake ni mkubwa na watanzania wengi zaidi wanatakiwa kuchangamkia kilimo hiki cha miti.
Kuanzisha Shamba La Kilimo cha Miti
Unapoanzisha shamba la miti ni muhimu kuzingatia mambo ya msingi katika kilimo cha miti kama vile aina ya miti, uchaguzi wa shamba la miti, usafi wa miti, uchimbaji wa mashimo ya miti pamoja na upandaji wako wa miche ya miti.
Unapokuwa makini tangu mwanzo katika kilimo cha miti unakuwa katika nafasi nzuri ya kuhakikisha kuwa miti yako itaota vizuri na kuwa na afya.
Tofauti na hapo ukuaji wa miti huwa hafifu na kupelekea hasara kubwa. Maandalizi sahihi ya miti huzalisha miti yenye ubora wa hali ya juu.
Mara baada ya kuchagua aina sahihi ya miti unayotaka kupanda, ni muhimu kuzingatia viwango vya mwinuko na mteremko pamoja na hali ya hewa. Nyanda za Juu Kusini zina udongo mzuri ambao unafaa kwa ajili ya kilimo cha miti ya aina nyingi ikiwemo mitiki, milingoti na mipaina.
Udongo wenye rutuba na uwezo wa kupitisha maji na kuyahifadhi kwa muda mrefu ni sifa kubwa katika ustawi wa miti kutokana na kwamba, miti inahitaji maji na virutubisho kutoka ardhini hivyo ni muhimu sana kuzingatia uwezo wa udongo.
Inashauriwa kupanda miti katika maeneo ambayo hupata millimita za ujazo 1,000 au zaidi ya mvua kwa mwaka.
Shamba la miti linaweza kuandaliwa kwa kulimwa na jembe la mkono, trekta au jembe la kukokotwa pia Inashauriwa kulima upana wa mita moja katika mstari wa kupanda miti au visahani vya upana wa mita moja.
Aidha, nafasi inayopendekezwa kutoka mti hadi mti ni mita 3×3 (hususani kwa mipaina) ili kuiwezesha kutanuka na kukua kwa haraka. Nafasi hii inaruhusu miti kupata mwanga na chakula cha kutosha.
Miti ya milingoti inaweza kupandwa nafasi ya mita 2.5×2.5 kwa sababu inahitaji kurefuka zaidi kuliko kutanuka.
Changamoto za Kilimo cha Miti
Pamoja na hayo, njia za kuzuia moto zinapaswa kutengenezwa kila mwaka mara baada msimu wa mvua kumalizika. Hii ni hatua muhimu kwa kufanya hivyo unapunguza hatari ya kupata hasara na upotevu wa eneo la uzalishaji.
Njia ya moto inaweza kuwa na upana wa mita tano hadi kumi kutoka shamba moja hadi jingine kwa sababu njia hizi hutumika kupitisha magari wakati wa mavuno.
Mikoa inayolima miti kwa wingi
Hapa nchini Tanzania mikoa ambayo imejikita zaidi katika kilimo cha miti ni pamoja na Iringa, Njombe, Mbeya na Kagera. Mkoa wa Iringa unaongoza kwa kuwa na misitu mikubwa ambayo imepandwa na serikali, mashirika kutoka nje ya nchi na watu binafsi.
Mavuno ya Kilimo cha Miti
Kwa mujibu wa wataalamu wa kilimo, heka moja ya shamba ina uwezo wa kuchukua hadi miti 600 ambapo wastani wa gharama ya mti mmoja uliokomaa ni kati ya Sh. 25,000 hadi Sh. 30,000, hivyo mkulima anaweza kuingiza hadi Sh. 18 milioni katika heka moja pekee ya shamba la miti.
Ikiwa umewekeza katika aina hii ya kilimo cha miti, ni muhimu sana kujua soko lako na kulima kulingana na mahitaji yaliyopo. Miti ya mipaina na milingoti inaelezwa kubwa na soko kubwa zaidi ndani na nje ya nchi.