Tabia za Watu Waliofanikiwa Kwenye Maisha

Mara nyingi watu hawa huwa na mfuatano au mpangilio mzuri na unaoeleweka wa kazi au maamuzi yao. Kwa kifupi watu hawa hufanikiwa sana na ndiyo huitwa watu waliojipanga.

1. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanaandika Kila Kitu

Kuandika vitu ni njia mojawapo ya kutekeleza mambo kwa mpangilio. Watu waliojipanga huandika mambo yote wanayotakiwa kufanya ili wasiyasahau na wanyafanye kwa wakati.

Watu waliojipanga hukagua pale walipoandika mara kwa mara ili kuona wamekamilisha lipi na lipi bado hawajakamilisha.

2. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanaweka Kitu Mahali Pake

Unapoweka kila kitu mahali pake, ni wazi kuwa ofisi au nyumba yako itaonekana imejipanga. Watu waliojipanga huweka kila kitu mahali pake hivyo hawapotezi muda wa kutenga siku ya kupangilia nyumba au ofisi.

Kwa mfano kama umeanua nguo, basi usizitupe kwenye kochi au kitandani bali zikunje au uzitundike. Unapomaliza kula pia usiache vyombo mezani bali vioshe uvihifadhi badala ya kuviacha mezani au kuvitelekeza jikoni.

Ukizingatia kuweka kila kitu mahali pake utakuwa mtu aliyejipanga zaidi.

3. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanagawa Majukumu

Watu waliojipanga hawajitutumui kufanya kila kitu; watu hawa hugawa majuku kwa watu stahiki. Badala ya kufanya kila kazi kwa ufanisi mdogo, ni vema ukagawa kazi hizo kwa watu wengine.

Kwa mfano ikiwa ni kwenye ngazi ya familia, mtoto mmoja anaweza kufagia, mwingine akadeki na wewe ukapika au kufanya shuguli nyingine muhimu.

4. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanapanga Kesho

Watu waliojipanga wanafahamu kuwa kesho haiandaliwi kesho bali leo. Hivyo hubainisha mapema majukumu wanayotakiwa kuyatekeleza kesho kwa kutegemea vipaumbele vyake.

Unapopanga kesho leo hukufanya kuwa na maandalizi mazuri na kuepuka kufanya mambo bila kuzingatia umuhimu wake.

5. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanafanya Kazi Kwa Bidii

Watu waliojipanga hufanya kazi kwa bidii ili wasije wakavuruga utaratibu au mpangilio wao. Hili ni kinyume kwa watu wasiojipanga kwani wao huahirisha mambo wakidhani kuwa wana muda mwingine.

Kwa kufanya kazi kwa bidii kunakufanya uwe na ratiba nzuri na inayoeleweka ambayo haiingiliwi na madeni ya kazi zilizoahirishwa.

6. Watu Waliofanikiwa Huwa Wana Ratiba na Wanaifuata

Tabia moja wapo ya watu ambao hawajajipanga ni kukosa ratiba, wao huamka na kufanya lile linalokuja mbele yao; au wakiwa na ratiba basi ni vigumu sana wao kuifuata.

Watu waliojipanga wana ratiba nzuri tena wanayohakikisha wanaifuata vyema. Ikiwa mtu aliyejipanga anatakiwa kuwa mahali au kukamilisha jambo fulani kwa wakati fulani basi hufanya hivyo bila kuacha.

7. Watu Waliofanikiwa Huwa Wana Vipaumbele

Watu waliojipanga wanafahamu ni nini cha muhimu zaidi kwenye maisha yao. Kwa kufahamu hili watu hawa huweza kuvipa vitu nafasi kulingana na umuhimu wake.

Watu wasiojipanga wanaweza kuangalia filamu (movies) au kukaa kwenye mitandao ya kijamii huku wakiacha majukumu yao ya msingi ya kila siku.

8. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanajali Afya Zao

Hakuna mafanikio au ufanisi katika jambo lolote kama hakuna afya nzuri. Watu waliojipanga wanafahamu wazi kuwa afya njema itawawezesha kufanya majukumu yao vyema, hivyo wanajali afya zao.

Ni wazi kuwa mtu anapougua majukumu au ratiba zake nyingi huvurugika au kukwama; hivyo kwa kulinda afya yako utaweza kutimiza majukumu yako kwa mpangilio uliojiwekea.

9. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanajiandaa Kwa Dharula

Dharula zipo kila mara kwenye maisha, na mara nyingi ndizo huvuruga ratiba za watu. Utasikia kauli kama vile nimepata dharula sitoweza kuja, nimepata dharura ndio maana sikumaliza, kuna kitu kilijitokeza, n.k.

Kwa hakika watu waliojipanga hujiandaa kwa dharula ili zisije zikavuruga mpangilio wao mzuri waliojiwekea.

10. Watu Waliofanikiwa Huwa Wanajali Muda

Kama nilivyoeleza kwenye hoja zilizopita, watu waliojipanga hawakubali kupoteza muda kwani kila muda wao una jukumu fulani kwenye ratiba.

Watu waliojipanga huamka mapema na huepuka tabia au matendo ambayo kimsingi yanapoteza muda.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

2 Comments
  1. Nimefurahi sana kiukweli na nimejifunza vitu vingi Sana kuhusu hizi tabia za watu waliofanikiwa.

Leave a reply

Wauzaji
Logo