
Mambo mapya ya kuzingatia na ambayo usiyoyajua kuhusiana na pesa pamoja na jinsi ya kutunza pesa kwenye maisha ya kila siku Tanzania
- Usikope pesa ya riba ili uanzishe biashara na Usitegemee pesa ya mkopo kuianzishia biashara, upate faida kisha uirudishe pesa ya mkopo na riba yake.
- Usitumie pesa ambayo bado haipo mikononi mwako na Wala usije ukamuahidi mtu kumpa pesa ambayo umeahidiwa mahali fulani.
- Kama unataka kutunza pesa, kila unapopata pesa usianze kuitumia kwanza kisha ukategemea kutunza kiasi kitakachosalia. Hivyo basi, ukipata tu pesa, weka pembeni kiasi unachodhani kinafaa kutunzwa kisha tumia kiasi kilichobaki.
- Ukipata nafasi ya kuonana na mtu tajiri, kamwe usiombe pesa. Omba maarifa ya kutengeneza pesa kama yeye, tena kwa mtaji mdogo. Maarifa ndio mtaji wa kwanza.
- Usitunze mbegu badala ya kuipanda. Watu wengi hufurahia pesa wanayopata kisha wanaiweka bank au nyumbani bila kuiwekeza. Wekeza pesa ili uzalishe zaidi. Usiogope kuingia hasara, kila aliefanikiwa alipoteza kwanza kabla hajafanikiwa.
- Kamwe usimkopeshe mtu pesa ambayo unahisi hatorudisha. Unapomkopesha mtu huyo pesa, jiridhishe mwenyewe moyoni kuwa kama hatoweza kulipa basi deni lake halitoathiri urafiki wenu.
- Usikubali uwe shahidi tena kwa kusaini kabisa ili umdhamini mtu ambae huna uhakika kuwa atalipa kile unachomdhamini. Kumbuka kuwa, dhamana maana yake utawajibika iwapo atashindwa kulipa.
- Epuka kutembea na pesa nyingi ambazo hata huna matumizi nazo wakati huo. Unaweza kujikuta unafanya matumizi ambayo hayakuwa kwenye ratiba sababu ya ushawishi wa pesa ya mfukoni.
- Epuka kutunza pesa mahali pasipo sahihi. Maeneo kama kwenye soksi, sidiria, chini ya mto wa kulalia, chini ya begi, kwenye kopo au hata kwenye begi la safari, si maeneo salama. Ni rahisi kusahau, kuibiwa au kupoteza pesa zako.
- Usitumie pesa kwa kitu ambacho hakikuwa kwenye ratiba yako. Jiulize kwanza kabla hujanunua, “Bila kitu hiki, maisha yataenda au lah? Ukiona maisha yataenda bila kitu hicho, acha kukinunua. Tabasamu kisha ondoka.
- Usiingiwe tamaa kwa kununua kitu ambacho ungeweza kununua kwa bei ya punguzo mahali pengine zaidi. Labda tu uwe una pesa nyingi.
- Matumizi yako ya pesa yasizidi pato lako. Unapaswa kuwa bahili katika matumizi yako. Cheza na pato lako. Fanya matumizi makubwa pale tu pato lako litakapoongezeka.