Sababu za Kufa Kwa Biashara Mpya Tanzania

Hakuna mtu anayeanzisha biashara akitegemea ife, lakini wakati mwingine hili hutokea pia Utafiti umebaini kuwa biashara na kampuni nyingi hufa ndani ya kipindi cha miaka miwili hadi mitano tangu kuanzishwa kwake.

Kufa kwa biashara Tanzania siyo jambo zuri, ni wazi kuwa kila mtu nayefanya biashara atatamani kufanya juu chini ili ainusuru biashara yake isife.

1. Biashara Nyingi zina Mipango duni

Ili ufanikiwe katika biashara unahitaji mpango mzuri wa biashara. Biashara nyingi zinazoanzishwa Afrika hazina mipango madhubuti ya kibiashara.

inayoonyesha maswala kama vile muundo wa utawala, mtaji, mikakati au mipango ya mauzo Biashara nyingi pia hukosa lengo jambo ambalo hufanya biashara nyingi kufa.

2. Biashara Nyingi zina Uongozi na usimamizi mbaya

Kufanikiwa kwa biashara kunategemea usimamizi mzuri. Uwekaji wa mipango na kuisimamia ili itimie hufanywa na uongozi mzuri.

Ni wazi pia rasilimali nyingi za kampuni zitapotea kutokana na kukosa uongozi na usimamizi mzuri. Biashara nyingi za Afrika huendeshwa kwa mazoea au kuendeshwa na watu wenye uwezo mdogo katika utawala.

3. Biashara Nyingi Haziwajali Wateja

Naamini unafahamu msemo usemao kuwa “Mteja ni mfalme”. Biashara nyingi za kiafrika hufa kutokana na kupuuza wateja pamoja na mahitaji yao.

Unaweza kuona mfanyabiashara anamjibu mteja vibaya au hamkaribishi kwa furaha bila sababu yoyote ya msingi. Wakati mwingine wafanyabiashara hawasikilizi maoni na mahitaji ya wateja jinsi ipasavyo.

Mfanyabiashara kujihisi kuwa yeye ndiyo mwenye faida kwa mteja ni kosa kubwa litakalogarimu biashara yake.

4. Biashara Nyingi Hazijifunzi kutokana na makosa

Makosa ni shule muhimu inayotuwezesha kuboresha viwango vya utendaji. Ni wazi kuwa yapo makosa yanayofanyika mara kwa mara kwenye uendeshaji wa biashara.

Wakati mwingine makosa haya huleta athari mbaya kwa biashara. Wafanyabiashara wengi hawapendi kujifunza kutokana na makosa haya ili wayaepuke mbeleni hivyo yanapotokea tena huwakuta hawajajiandaa vyema.

5. Biashara Nyingi Huwa zinajipanua bila mipango

Upanuzi wa biashara ni jambo linalohitaji mipango madhubuti. Kuongeza ukubwa wa biashara kunahitaji kutazama mambo kama vile mtaji, watumishi, vitendeakazi, uendeshaji na usimamizi na masoko.

Biashara nyingi hujipanua bila kutazama mambo haya; jambo ambalo linapelekea biashara nyingi kufa.

6. Biashara Nyingi zimechagua Eneo Baya La Biashara

Uchaguzi mbaya wa eneo la kibiashara hupelekea biashara nyingi kufa kutokana na kukosa wateja. Biashara nyingi hushindwa kubainisha eneo ambalo linafaa kwa ajili ya biashara zao na hatimaye hukosa wateja na kufa.

Kwa mfano kufungua biashara ya kuuza vifaa vya magari katikati ya soko la vyakula ni wazi kuwa mauzo yatakuwa duni sana.

7. Biashara Nyingi Hukosa faida

Biashara ni lazima iwe na faida ili isife. Kama biashara inauza bidhaa za shilingi 10,000 ni lazima pia ipate zaidi ya 10,000 katika mauzo yake.

Wafanyabiashara wengi hujifariji kuwa kufanya biashara bila faida ni jambo la kawaida. Ni kweli swala hili linaweza kutokea lakini lisiwe ni swala la mazoea.

Ni muhimu kuhakikisha biashara inatengeneza faida ili iweze kujiendesha vyema.

8. Biashara Nyingi zina Usimamizi mbaya wa fedha

Usimamizi wa fedha ni tatizo kubwa linaloua biashara nyingi. Hili linatokana na maarifa duni ya utunzaji wa pesa pamoja na tabia ya baadhi ya watumishi kukosa uaminifu katika swala la kusimamia na kutunza pesa.

Watu hawajui kutunza pesa zao binafsi, hivyo hata wanapokabidhiwa pesa za biashara huzitumia hovyo hovyo.

9. Biashara Nyingi zina Washirika Wabaya wa Kibiashara

Mshirika mzuri wa kibiashara ni yule anayeweza kukuunga mkono katika maono na malengo yako ya kibiashara.

Biashara nyingi hufanya kazi na washirika wabaya wasioweza kuendeleza maono na malengo ya biashara husika hili husababisha biashara nyingi kukwama kwa kukosa ushirikiano stahiki.

10. Biashara Nyingi Hufa Kwa Mambo Yasiyo Ya Kiuchumi

Kuna mambo yanayoweza kuua biashara ambayo mengi siyo ya kiuchumi na mara nyingi hayazuiliki. Maswala kama vile majanga ya asili (mafuriko, ukame na tetemeko), mabadiliko ya hali ya uchumi wa nchi na dunia, sera mbovu za kisiasa na vita, n.k.

Ni baadhi ya mambo ambayo yanaweza kusababisha biashara kufa. Pamoja na hali hii biashara mbalimbali zinaweza kuweka mipango mapema ya kujiokoa katika hali hizi kama vile kuhakikisha uwepo wa akiba ya kutosha ya rasilimali hasa fedha.

11. Biashara Nyingi zina Mbinu Duni za Masoko

Masoko ni taaluma rasmi inayofanywa na watu waliofuzu vyema. Ni tatizo kubwa sana kupuuza swala la masoko.

Biashara nyingi hazifahamu jinsi ya kutafuta na kutawala soko, hivyo hujikuta wakipoteza soko la bidhaa zao na hatimaye kufa kwa kukosa mapato.

Ni muhimu kujifunza mbinu sahihi za masoko kulingana na bidhaa na wakati husika.

12. Biashara Nyingi zina Ajiri Watumishi Duni

Biashara nyingi hupendelea watumishi duni (cheap labour) ili wawalipe malipo kidogo. Ni ukweli usiopingika kuwa mtumishi duni atafanya kazi duni.

Biashara nyingi hazioni mafanikio wala matokeo chanya, kutokana na kuajiri watu wasiokuwa na uwezo wala ubunifu wa kufanya biashara husika kwa njia yenye tija.

Ni heri kuajiri mtumishi mmoja bora kuliko watano duni.

13. Biashara Nyingi Zinakumbana na Matatizo Ya kisheria

Kuna wakati biashara au kampuni huingia kwenye matatizo ya kisheria yanayoigharimu biashara au kampuni husika fedha nyingi. Migogoro na matatizo haya yanaweza hata kupelekea kufilisiwa kwa biashara husika.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply

Wauzaji
Logo