Mambo Ya Kuzingatia Unapochagua Mpenzi

Jinsi ya kuchagua mchumba ni swala nyeti linalohitaji maamuzi yanayohusisha hekima, utulivu, kumwomba Mungu pamoja na uchunguzi wa kutosha.

Maisha ya watu wengi yamekuwa na matatizo makubwa kutokana na kufanya makosa katika kuchagua mtu wa kuoa au kuolewa naye.

Kwa hakika hakuna mwenzi mkamilifu, lakini kuna sifa za msingi ambazo kila mtu unayetarajia kuoa au kuolewa anapaswa kuzizingatia na kuzitilia maanani.

1. Jitahidi Kuchagua Mtu Mwenye Malengo

Hakikisha mtu unayetaka kuoana naye ni mtu mwenye malengo katika maisha yake. Mtu mwenye malengo hujishughulisha kila mara kuhakikisha anaandaa baadaye yake.

Mtu asiyekuwa na malengo huwaza matumizi na anasa kuliko kuzalisha au hafanyi kazi wala hajali kuhusu kesho Hakika mtu kama huyu hawezi kuingia kwenye ndoa ikadumu au akaweza kulea familia yenye ustawi mzuri.

2. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaekuheshimu

Heshima na kuthaminiana ni msingi muhimu katika ndoa. Nimeshuhudia mwanandoa akimzarau au hata kumbeza mwenzi wake mbele ya wageni au watoto ni wazi kuwa tabia hii ilianza siku nyingi.

Ni muhimu kuhakikisha mtu unayetaka kuoana naye anathamini utu wako kuliko hata vitu vingine. Hakikisha anakusikiliza na kujali pia hisia zako.

3. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaejali Ndugu Zako

Ndoa ni kitu kinachounganisha watu wengi, watu wanapoingia kwenye ndoa familia mbili huungana kupitia ndoa hiyo.

Hivyo ni muhimu kuhakikisha mtu unayetaka kuoana nae anathamini na kuheshimu familia yako. Naamini usingependa mama, baba, shangazi, mjomba au ndugu yako wa damu adharauliwe na mwenzi wako.

Hivyo chunguza msimamo na tabia ya yule unayetaka kuoana naye ukoje juu ya familia yako kabla hamjaoana.

4. Jitahidi Kuchagua Mtu Ambaye Anakuamini

Migogoro mingi kwenye ndoa inatokana na wanandoa kutokuaminiana. Kamwe usikubali kuoana na mtu ambaye hakuamini vyema.

Nimeshuhudia watu wakiwekewa watu wa kuwafuatilia, simu zao zikifuatiliwa na hata kuwekewa sheria kali kutokana na mwenzi mmoja kutokumwamini vyema mwenzake.

Kumbuka! Kama anakupenda kweli atakuamini na kuwa mwaminifu kwako.

5. Jitahidi Kuchagua Mtu Ambaye Anaekupenda

Watu wengi hutamaniana badala ya kupendana. Tamaa huongozwa na vitu au mwonekano wa nje tu.

Hakikisha unaoana na mtu ambaye hata ukiwa mgonjwa, mzee, maskini au dhaifu bado atakupenda tu jinsi ulivyo. Kumbuka pia upendo wa kweli hautaki malipo wala hauulizi kwanini.

Tamaa huhusisha hisia kali  na baada ya muda hisia hizi hutoweka na kuisha kabisa ila upendo huhusisha bidii, kujitoa, kuvumilia na akili nyingi.

6. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaemheshimu Mungu

Watu wengi hupuuza nafasi ya Mungu katika mahusiano na maisha yao kwa ujumla. Ni muhimu ukakumbuka kuwa kwa asili binadamu hakuumbwa kukaa bila imani ya kitu chochote.

Mwenzi mwenye hofu ya Mungu atakujali, atakuheshimu, atakuthamini, atakutia moyo, atakuombea na hata kulea familia katika maadili mema.

7. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaekufanya Ufurahi

Kuna watu wanakaa kwenye mahusiano na watu ambao hawawapi furaha lakini bado wanaendelea kung’ang’ania hadi ndoa Inawezekana hiii ni kutokana na upendo kujengwa kwenye vitu kama vile pesa.

Kumbuka kuwa hakuna mbadala wa ndoa, ukishaingia umeingia; hivyo hakikisha mtu unayeoana nae anakufanya ufarahi kila mara na si uhuzunike maana utahuzunika maisha yako yote.

8. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaekusaidia Kuwa Bora Zaidi

Je ulikua hujui kuvaa akakufundisha kuvaa? Ulikuwa hujui kupika akakufundisha kupika? Au umejifunza vitu vipya kutoka kwake?

Ni muhimu ukajiuliza maswali kama haya ili uweze kupata mwenzi wa maisha ambaye anaweza kukufanya kuwa bora zaidi na si kukurudisha nyuma au kukuacha ulivyo.

9. Jitahidi Kuchagua Mtu Ambaye ni Msikivu

Usikivu ni tabia muhimu sana kwenye ndoa. Hakikisha yule unayetaka kuoana naye ana usikivu mzuri. Uwekaji na utekelezaji wa mipango mbalimbali katika familia unategemea kusikilizana.

Hebu fikiri baba anataka kujenga wakati mama anataka kununua gari, baba anataka mama asimamie miradi wakati mama anataka kwenda kusoma; ni wazi kuwa hapa kutakuwa na sitofahamu kubwa.

10. Jitahidi Kuchagua Mtu Ambae Anasamehe

Watu wanapokaa pamoja, kukoseana hakuepukiki. Hivyo ni muhimu kumchagua mwenzi wa maisha ambaye anajua umumu wa kusamehe.

Epuka kuoana na mtu mwenye tabia za kubeba vinyongo na chuki kwani mtashindwana mapema kwenye ndoa.

11. Jitahidi Kuchagua Mtu Asiye na Tamaa

Mapenzi ya leo kwa kiasi kikubwa hujengwa kwenye vitu na mali. Wengi hupendana kutokana na pesa au mionekano ya nje tu; hili limesababisha wengi kutengana pale vitu hivyo vinapokosekana.

Hakikisha kama unataka kuoana na mtu sahihi unatafuta mtu ambaye upendo wake haujajengwa kwenye vitu vya muda vinavyopita.

12. Jitahidi Kuchagua Mtu Mwenye Shukrani

Mtu asiye na shukurani ni mtu asiyefaa kuwepo kwenye ndoa. Watu hawa huwa hawaoni jema wala zuri lolote, wao ni kulalamika na kulaumu tu.

Hakikisha unaoana na mtu mwenye shukurani hata kwa mambo madogo, kwani kwa kufanya hivi mtakuwa na ndoa yenye upendo na kuthaminiana kila mmoja.

13. Jitahidi Kuchagua Mtu Ambaye Sio Mzinifu

Watu wengi hujenga mahusiano yao kwenye tendo la ndoa, jambo linalowafanya wengi kuishia kuzaa nje ya ndoa au hata kutokuwa tayari kuingia kwenye ndoa kwani mambo yote ya ndoa tayari yameshafanywa.

Mtu anayekuthamini hatakutaka kimwili bali atauthamini mwili na utu wako hadi mtakapokuwa kwenye ndoa kamili. Wakati fulani nilisoma mtandaoni kuwa “Vijana wengi wa kiume hawafanyi maamuzi ya kuoa kwa kuwa ngono inapatikana kirahisi”

Kumbuka! Kukutana kimwili siyo tiketi ya kuolewa na mtu; mnaweza kukutana kimwili na bado akakuacha, hivyo kuwa makini.

14. Jitahidi Kuchagua Mtu Mkarimu

Mwenzi mkarimu ni bora kwani atakuwa mkarimu kwako, familia yako pamoja na wageni watakaofika nyumbani kwenu.

Unapooana na mwenzi mchoyo ni wazi kuwa ataharibu mahusiano yako na watu; wala hatakuwa tayari kukuhudumia wewe au mtu mwingine kupitia vitu mlivyonavyo.

15. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaekutia Moyo

Moja ya jukumu muhimu la mwenzi wa maisha ni kukutia moyo hasa pale unapokutana na changamoto. Hakikisha unaoana na mtu anayeweza kubeba raha na mamumivu yako.

16. Jitahidi Kuchagua Mtu Anaetumia Pesa Vyema

Mwenzi asiyejua kutumia muda na pesa vyema ni mzigo na hasara kubwa. Ili mtu afanikiwe ni lazima ajifunze umuhimu wa kujali muda pamoja na matumizi mazuri ya pesa.

Hebu fikiri mke anayekaa kwenye televisheni siku nzima au mume anayeshinda kijiweni; niwazi hawa watakuwa masikini na hawataweza kulea familia zao katika malezi bora.

Hakikisha unaoana na mtu anayetunza pesa na muda vyema.

17. Jitahidi Kuchagua Mtu Mwenye Ukomavu wa Akili

Siyo kila mtu ana akili iliyokomaa kuingia kwenye ndoa. Watu wengine bado ni watoto wadogo ambao hata maaumuzi na matendo yao bado ni ya kitoto.

Ndoa ni swala linalohitaji akili iliyokomaa vyema inayoweza kufanya maamuzi sahihi pamoja na kupambanua jema na baya. Hivyo hakikisha unaoana na mtu mwenye upeo mzuri wa kufikiri.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply