Mambo Ya Kuzingatia Kwenye Logo Ya Biashara

Logo ni utambulisho wa biashara, kampuni yako au bidhaa Hivyo, Logo ni moja kati ya mambo makuu ambayo yanafanya biashara yako kukumbukwa na kutambulika.

Makampuni na watu mbalimbali wamekuwa wakiwekeza fedha nyingi ili kupata Logo bora Pamoja na kuwekeza pesa nyingi, bado kampuni na watu wengi hawapati Logo bora.

1. Jitahidi Kuepuka Kuchagua Logo inayofanana na Nyingine

Ni rahisi kujikuta unatengeneza Logo inayofanana na ya kampuni au mtu mwingine. Hili linaweza kusababishwa na mambo kama vile kutumia programu au mfumo wa aina moja kutengeneza Logo husika; pia linaweza kusababishwa na kutaka kwa makusudi kufananisha Logo ili utambulike haraka.

Hili ni kosa baya, kwani linaweza kukuletea matatizo mbalimbali kama vile mgogoro wa kisheria wa hakimiliki pamoja na kuwachanganya wateja.

2. Jitahidi Kuepuka Uchaguzi Mbaya wa Rangi

Watu wengi hawajui kuchagua na kutumia rangi mbalimbali ipasavyo. Hili huwasababisha watu wengi kushindwa kufahamu maana ya rangi husika na kama inafaa au laa katika Logo zao.

Ni vyema ukazingatia haya:

  • Maana ya rangi husika.
  • Ubora wa rangi husika.
  • Kufaa kwa rangi katika matumizi mbalimbali kama vile kazi za uchapishaji, mtandao, video na picha Ni vyema ukahakikisha kuwa rangi ya Logo itafaa kwenye kazi tajwa hapo juu na nyinginezo.

Naamini ukizingatia haya utaweza kuchagua rangi itakayofaa kulingana na kazi au biashara yako.

3. Jitahidi Kuchagua Mwandiko Mzuri

Kama ilivyo kwa rangi, mwandiko una umuhimu na maana kubwa kwenye Logo yako. Hivyo ni vyema ukachagua mwandiko bora utakaokidhi matumizi na kuitambulisha biashara yako vyema.

Hakikisha mwandiko wako ni wa kipekee, haumilikiwi kisheria na mtu au kampuni nyingine pia unasomeka vyema katika matumizi yote.

4. Jitahidi Kuepuka Kuweka Kila Kitu Kwenye Logo

Ni kweli kuwa Logo ni kitambulisho cha biashara au kile unachokifanya, lakini haiwezi kueleza kila kitu. Hakikisha Logo yako haina vitu vingi visivyokuwa na sababu.

Hakikisha inaeleweka vyema bila tatizo lolote. Kwa mfano kama kauli mbiu (slogan) yako ni ndefu sana, basi hakuna haja ya kuiweka kwenye Logo yako.

5. Jitahidi Kuepuka Kuweka Matukio Ya Muda Mfupi

Mara nyingi kuna watu na matukio yanayoibuka kwa muda fulani. Si vyema kuhusisha matukio au watu hawa katika Logo yako; kwani ni muhimu kutengeneza Logo itakayofaa muda mrefu au wote.

Kwa mfano Logo kama vile “Kanumba Barber Shop”, “Spartan Studio”, “Prison Break Elctronics” “Obama Supermarket” ni baadhi tu ya mifano ya Logo ambazo zimehusisha matukio na watu wa muda.

Matukio haya yatakapopita na Logo yako itakuwa pia imepitwa na wakati.

6. Jitahidi Kuepuka Logo Zenye Maumbo Yasiyoeleweka

Yapo maumbo yanayopatikana katika programu mbalimbali za kutengenezea logo; maumbo mengine hayana maana inayoeleweka yaani yana maana dhahania tu (maana inayofahamika na mbunifu pekee).

Unapotumia maumbo kama haya ni rahisi kumchanganya mtu anayeona Logo yako, kwani hataweza kupata maana au ujumbe lengwa.

Tumia maumbo ambayo yanasadifu kile kinachofanywa na kampuni au bidhaa yako.

7. Jitahidi Kuikagua Logo Yako Vizuri

Ni vyema ukafahamu kuwa kazi ya kibunifu na kitaalamu ni lazima ihaririwe. Ni vyema ukahariri kwa makini Logo yako ili kuhakikisha haina makosa kama vile makosa ya spelling.

8. Jitahidi Kuepuka Kuweka Symbol

Alama kama TM, LLC, INC au LTD kwenye Logo yako hakuifanyi Logo kuwa ya kisasa bali ya kizamani. Hii ndiyo sababu hata google wameondoa alama hizi katika Logo yao.

Mara nyingi alama hizi huwa hazionekani au kusomeka vyema kwenye maeneo ambayo Logo inatumika kwa vipimo vidogo.

9. Jitahidi Kuepuka Kutumia Huduma za Logo za Bure

Mara nyingi kutengeneza Logo kwa kutumia huduma au programu za bure, kunakufanya utengeneze logo ambayo siyo ya kipekee.

Hili linatokana na watu wengi kupendelea na kutumia huduma hizi. Kosa hili linaweza pia kukusababisha kuingia kwenye migogoro ya kisheria na watu au kampuni nyingine.

10. Jitahidi Kuepuka Logo Ambayo Haina ubunifu

Kutengeneza Logo ni kazi nyeti ambayo inahitaji ubunifu na uzoefu mzuri ili kuwa na matokeo mazuri. Ni ukweli usiopingika kuwa hii ndiyo sababu watu hulipwa kiwango kikubwa cha pesa ili kutengeneza nembo mbalimbali.

Watu wengi wamekuwa wakijikuta wakitengeneza Logo mbaya kutokana na kukosa ubunifu. Ninakushauri ikiwa unaona ni vigumu kutengeneza Logo yako mwenyewe ni vyema ukamtumia mtu mwenye uwezo mzuri wa ubunifu.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply

Wauzaji
Logo