Mambo Ya Kuzingatia Kabla Ya Kununua Kiwanja Tanzania

Kiwanja ni rasilimali muhimu Tanzania ambayo kila mtu anaihitaji kwa namna moja au nyingine na Watu wengi hununua ardhi kwa ajili ya kufanyia shughuli mbalimbali kama vile ujenzi na kilimo.

Pamoja na umuhimu huu mkubwa wa ardhi bado watu wengi wanakumbana na changamoto mbalimbali katika maswala yanayohusu kununua na kumiliki ardhi.

Wengi hujikuta wakinyang’anywa viwanja vyao, kuharibiwa mali, au wakiingia kwenye migogoro mikubwa ya kisheria.

1. Jitahidi Kuona Kiwanja Husika Wewe Mwenyewe

Ni vyema ukafika kwenye eneo la kiwanja husika na kukiona wewe mwenyewe kama kinakuridhisha na kukufaa kwa mahitaji yako.

Fahamu mipaka, na vitu vingine vinavyohusu kiwanja kama vile mimea iliyopo, aina ya udongo n.k. Kwa kufanya hivi utaweza kubaini kama kiwanja kinakidhi mahitaji na matumizi yako.

2. Jitahidi Kumfahamu Mmiliki Halisi wa Kiwanja

Matatizo mengi yanayowakumba watu kwenye maswala ya ardhi ni kutokana na kuuziwa ardhi na mtu ambaye si mmiliki halisi wa ardhi. Ni muhimu sana, tena sana, ukamfahamu mmiliki halisi wa ardhi unayotaka kuinunua kabla hujainunua. Kama ardhi imesajiliwa unaweza kwenda wizara ya ardhi ili kufahamu mmiliki halisi.

Pia ni lazima ufahamu kama kiwanja au ardhi kinamilikiwa na wanandoa (matrimonial property) ili upate ridhaa ya familia juu ya kununua kiwanja husika. Mara nyingi watu hasa wanaume huuza viwanja vya familia kwa siri bila kushirikisha familia; jambo ambalo linaweza kukuingiza kwenye mgogoro mkubwa na familia husika. Kwa kumfahamu mmiliki halisi utaweza kuepuka migogoro au kupoteza pesa zako.

3. Jitahidi Kuwaepuka Madalali wa Viwanja

Karibu kila kinachouzwa leo kuna madalali. Madalali hawana cha ziada zaidi ya kutafuta njia za ujanja ujanja za kupata pesa.

Kama kiwanja kinauzwa milioni 5 dalali anaweza kukuambia milioni 7 ili apate zake 2 Hivyo ni muhimu kumtafuta mwenye mali halisi ili uzungumze na kupatana naye kuhusu gharama halisi za kiwanja.

Kwa kufanya hivi utaokoa pesa zako ambazo zingechukuliwa na madalali.

4. Jitahidi Kuangalia Uwepo wa Huduma za Kijamii

Uwepo wa huduma za kijamii katika eneo husika ni muhimu sana, lakini watu wengi huwa hawazingatii hili.

Ni muhimu kabla hujanunua kiwanja ukaangalia uwepo wa huduma kama vile maji, hospitali, barabara, soko, shule na nyumba za ibada.

Hili litakuwezesha hasa kama unataka kuishi eneo husika kupata huduma za kijamii kwa karibu bila shida wala gharama ya ziada.

5. Jitahidi Kuchunguza Migogoro Ya Kisheria

Kutokana na makosa mbalimbali yanayofanyika kwenye maswala ya ardhi, ardhi nyingi sana hivi leo zina migogoro ya kisheria.

Ni vyema ukajiepusha kujitumbukiza kwenye kesi na matatizo yasiyokuwa ya lazima kwa kununua kiwanja au ardhi yenye mgogoro wa kisheria.

Unaweza kulibaini hili kwa kufanya uchunguzi wa kina kabla hujanunua ardhi husika.

6. Jitahidi Kuchunguza Kama Kiwanja Kimewekwa Rehani

Viwanja na mashamba huwekwa rehani kwa taasisi mbalimbali hasa zile za kifedha. Watu wenye nia mbaya huuza viwanja vilivyowekwa rehani.

Kununua kiwanja hiki kutakuingiza kwenye mgogoro na taassisi husika. Na kwa sababu taasisi hii inakihodhi kisheria, hutoweza kukipata kiwanja husika bali unaweza kupoteza fedha zako.

7. Jitahidi Kufahamu Hali Ya Kijografia Ya Eneo

Nimeshuhudia watu wakiuziwa viwanja kwenye mikondo ya maji pamoja na matindiga hali inayowapelekea kupata adha kubwa wakati wa mvua.

Ni vyema ukafahamu hali ya kijografia ya kiwanja au ardhi unayoinunua.

Hakikisha mambo yafuatayo:

  • Eneo husika siyo tindiga au kinamasi
  • Eneo husika siyo mkondo wa maji – unaweza ukazolewa na mafuriko hapa.
  • Eneo husika siyo bonde linalojaa maji
  • Eneo husika siyo eneo la magadi
  • Siyo eneo la maporomoko ya ardhi
  • Siyo eneo lenye ardhi inayotitia n.k

Kwa kutazama baadhi ya mambo kama haya ya msingi, utaweza kuhakikisha unanunua eneo zuri na salama kijografia.

8. Jitahidi Kuchunguza Ramani Ya Mipango Miji

Kuna maeneo ya ardhi yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli maalumu. Maeneo hayo yanaweza kuwa ni ya miradi ya serikali, maeneo ya wazi, hifadhi ya barabara, hifadhi ya wanyama pori, chanzo cha maji au hata ardhi ya kampuni au taasisi fulani.

Watu wengi wamenyang’anywa ardhi zao au hata pengine kuharibiwa mali zao kwa kosa la kujenga au kufanya shughuli katika maeneo haya.

Pia unaweza kwenda kwenye ofisi zinazoshughulika na maswala ya ardhi na mipango miji ili kupata taarifa kamili.

Inashauriwa kuchunguza ardhi vyema kabla ya kuinunua ili uweze kubaini maswala haya.

9. Jitahidi Kufahamu Kama Kuna Mpangaji

Kuna watu wanakodisha ardhi kwa ajili ya shughuli na miradi mbalimbali kwa kipindi fulani cha muda. Hivyo kabla ya kununua ardhi hakikisha kuwa hakuna mkodishaji au mmepatana naye kwanza.

Ni vigumu kumtoa mtu aliyekodisha ardhi na kuilipia kwa miaka kumi kwa kigezo tu kuwa umeinunua. Hivyo kuwa makini na chunguza swala hili kabla.

10. Jitahidi Kumuhusisha Mwanasheria

Kutokana na ukosefu wa elimu pamoja na hali ya mazoea, watu hujimilikisha ardhi bila kufuata taratibu za kisheria.

Ni lazima ufahamu kuwa ardhi ni kitu kinachomilikiwa kisheria Hivyo ni lazima makabidhiano au manunuzi ya ardhi yazingatie sheria na kuhusisha ushahidi wa kisheria kama inawezekana.

Unapomhusisha mwanasheria katika manunuzi yako ni wazi kuwa utajiwekea uhakika wa kuwa mmiliki halali kwani umefuata taratibu za kisheria.

Zipo taasisi nyingi unazoweza kuziona na ukapata usaidizi wa kisheria bure au kwa bei nafuu.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply

Wauzaji
Logo