Kilimo Cha Mananasi Tanzania

Kilimo cha Mananasi Tanzania ni moja ya kilimo maarufu na hupendwa na walaji wengi hapa Tanzania kwasababu ya ladha yake tamu na harufu yake nzuri.

Tunda hili laweza liwa mara tu baada ya kuvunwa, baada ya kulipika, au kama juisi. Nanasi ni chanzo kizuri cha vitamin A na B, pia inakiwango kingi tu cha vitamin C.

Asili kilimo cha mananasi inaaminika kuwa ni Brazil na Paraguay huko Amerika ya Kusini kwa Hapa Tanzania, mananasi hulimwa zaidi maeneo ya Bagamoyo, Kibaha (Pwani), Tanga, Mtwara, Lindi, Geita na Mwanza.

Lakini pia maeneo yote ya pwani ya Tanzania yanafaa kwa kilimo cha nanasi.

Hali Ya Hewa Inayofaa Kwa Ukuaji wa Nanasi

Kilimo cha nanasi kinapendelea hali ya hewa ya joto na husitawi vema katika mwinuko kati ya mita 0-1750 kutoka usawa wa bahari. Mwinuko wa mita 1300 hadi 1750.

Mahitaji ya joto ni kati ya nyuzi joto 18°C hadi 35°C.

Udongo Unaofaa Kwa Kilimo Cha Nanasi

Kwa kilimo cha nanasi chachu (pH) ya udongo inayofaa ni 5.5 hadi 6.0, na hustawi vizuri zaidi katika udongo tifutifu na udongo wenye kichanga usiotuamisha maji.

Ingawa nanasi huweza kustawi katika udongo wa aina yoyote ile, ila udongo wa mfinyanzi haufai kwa kilimo cha nanasi.

Maandalizi Ya Shamba la Mananasi

Lima shamba la mananasi kwa trekta, kwa ng’ombe ama kwa jembe la mkono kwa kina cha sentimita 30 hadi 45. Shamba la nanasi unaweza kulilima kwa sesa (flat-bed) au kwa matuta (furrows).

Weka mbolea kianzio katika kila shimo na upande, hakikisha shamba lina unyevu wa kutosha kabla ya kupanda. Weka tani 10 hadi 15 za mbolea ya kuku, weka pia viganja 2 vya mbolea ya zizi katika kila shimo.

Upandaji wa Mananasi

Zipo aina mbali mbali za mbegu za nanasi lakini yale yanayochipua kutoka ardhini hufaa zaidi na hukomaa mapema.

Chagua machipukizi mazuri ya nanasi yenye umri mdogo na yenye kulingana kwa ukubwa. Iweke miche kwenye kivuli kwa siku 3 kabla ya kuipandikiza iweze kutoa mizizi haraka.

Pandikiza mwanzoni mwa mvua za masika. Nafasi iwe cm 60 kati ya mistari, cm 30 kati ya miche na cm 80 kati ya mistari miwili.

Pandikiza miche 50,000 katika hekta moja. Chovya miche kwenye dawa ya Diazinon au Fention kwa muda wa dakika 25 kabla ya kuipandikiza ili kuzuia mashambulizi ya wadudu.

Palizi Kwenye Shamba La Nanasi

Palilia shamba la mananasi mara kwa mara ili kuhakikisha shamba halina magugu. Katika kilimo cha nanasi magugu hudhibitiwa kwa palizi ya jembe, kung’oa kwa mkono ama matumizi ya viuagugu.

Matumizi ya viuagugu hurahisisha zaidi palizi ya nanasi ukizingatia kuwa nanasi huwa na miiba katika ncha za majani yake ambazo huchubua ngozi endapo palizi za jembe zitatumika.

Njia nyingine ni matumizi ya matandazo (mulch) ya majani au plastiki (plastic mulch) maalum kuzuia magugu.

Jinsi Ya Kuweka Mbolea Kwenye Mananasi

Weka mbolea ya NPK gramu 50 hadi 70 kwa kila mche wakati wa kupanda. Weka tena gramu 85 kwa kila mche baada ya miezi 3 na pia miezi 3 baadae.

Wadudu na Magonjwa Yanayosumbua Mananasi

Mananasi ni zao lisilosumbuliwa na wadudu ama magonjwa mara nyingi. Hii ni faida kubwa sana kwa wakulima wa nanasi.

Hivyo endapo patatokea mashambulizi ya wadudu na magonjwa, ushauri zaidi wa kitaalam utafutwe kukabiliana na tatizo husika.

Hakikisha unakagua shamba ili kuzuia wadudu kama wataonekana.

Uvunaji wa Kilimo cha Mananasi

Nanasi huanza kutoa maua miezi 12 hadi 15 baada ya kupanda kutegemeana na aina ya nanasi au maotea ya mbegu yaliyotumika, muda wa kupanda na joto la mahali husika.

Kwa kawaida nanasi hukomaa miezi 5 baada ya kutoa maua, hivyo nanasi huchukua miezi 18 hadi 24 mpaka kukomaa na kuiva.

Katika kilimo cha nanasi, mimea ikitoa maua kwa nyakati tofauti tofauti itasababisha kuvuna kidogo kidogo na kwa muda mrefu.

Kwa sababu hiyo ndio maana ni muhimu kupanda kwa wakati mmoja mbegu zenye umri na ukubwa sawa.

Kwa wanaofanya kilimo cha mananasi kibiashara hutumia kemikali aina ya Ethrel mwezi mmoja kabla ya kuanza kutoa maua ili mimea mingi iweze kutoa maua kwa wakaii mmoja, angalau 80% ya mimea yote.

Vuna wakati kikonyo cha nanasi kimebadilika rangi kuwa njano ya dhahabu. Kata kikonyo cha nanasi chenye urefu wa cm 30 kikiwa kimeshikana na nanasi na upunguzie majani ya kichungi chake.

Utunzaji wa Mananasi

Hifadhi nanasi katika eneo lenye ubaridi huku kikonyo chake kikielekea juu. Hakikisha unauza nanasi mara tu au siku 2 hadi 3 baada ya kuvuna ili kutunza ubora wake.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply