Kilimo Cha Binzari Tanzania

Kilimo cha binzari Tanzania asili yake ni Mashariki ya Mbali, na hulimwa zaidi katika mkoa wa Tanga, Kagera, Kilimanjaro, Morogoro na Zanzibar. 

Mahitaji Kwenye Kilimo Cha Binzari

Hali Ya Hewa

Binzari Humea vizuri maeneo yenye kiasi cha joto la nyuzi 24-26 za sentigredi na huzalishwa maeneo ya mwambao.

Udongo Mzuri wa Binzari

  • Udongo wenye rutuba na unaopitisha maji na usio na mawe au changarawe.
  • Mahitaji ya mvua ni milimita 1200-2000 kwa mwaka.
  • Epuka kusimama kwa maji shambani ila Umwagiliaji unaweza kufanywa endapo maji hayatoshelezi.
  • Binzari inafanya vizuri ikipandwa sehemu ya uwazi Ingawa pia inaweza kuchanganywa na mazao mengine kama minazi.

Uchaguzi wa mbegu za Binzari

Mbegu za binzari zinazotumika hapa nchini ni za kienyeji bado. Tunguu kubwa zenye ukubwa wa sm 2.5 hadi sm 3 hutumika kama mbegu.

Kiasi cha tani 1.7 za vipando huhitajika kwa hekta. Tunguu za kupandwa zisihifadhiwe kwa zaidi ya mwezi mmoja kabla ya kupanda.

Nafasi ya upandaji wa Binzari

Nafasi ya kupanda binzari ni sm 15-25 kati ya mmea na mmea na sm 25-30 kati ya mstari na mstari au sm 45-60 kati ya tuta na tuta.

Mahitaji ya mbolea za Binzari

Matumizi ya mbolea hapa Tanzania si makubwa katika kilimo cha viungo. Tafiti zimeonesha kuwa binzari hazioneshi kufanya vizuri kwenye mbolea za viwandani.

Mbolea za samadi zinaweza kutumika. Kiasi cha tani mbili hadi tatu za samadi kwa eka moja kinatosha.

Uvunaji wa zao La Binzari

Uvunaji hufanywa kwa kutumia majembe au uma. Binzari huvunwa wakati majani yamegeuka rangi na kuwa njano au kahawia.

Binzari isiyo na kambamba huvunwa kipindi cha miezi sita toka kupandwa na miezi 18 hadi 21 kwa binzari iliyokomaa kutegemeana na mahitaji ya soko.

Mavuno ya tani 7 hupatikana endapo binzari ikipandwa peke yake. Mavuno hupungua kiasi binzari ikipandwa mchanganyiko na mazao mengine kwa mfano mavuno ya tani 4.8 kwa hekta yatapatikana binzari ikipandwa na minazi.

Utayarishaji wa Binzari

Kabla ya kuhifadhiwa binzari zichemshwe kwa dakika 45 hadi saa moja ili kuondoa harufu yake ya udongo. Pia kuchemsha kunasaidia zikauke kwa pamoja.

Binzari zichemshwe  mpaka kijiti kisicho na ncha kali kiweze kutoboa kwa urahisi Kisha ziepuliwe na kuanikwa juani kawaida huchukua siku 10 hadi 15 ili zikauke kufikia kiasi cha unyevu 5% hadi 10%.

Binzari pia yaweza katwa vipande vidogo vidogo ili kurahisisha kukauka Baada ya hapo ziko tayari kutwangwa au kusagwa kwenye mashine za kusagia viungo au kuhifadhiwa kama zilivyo.

Wadudu na magonjwa Ya Binzari

Tatizo kubwa ni ugonjwa wa ukungu unaosababishwa na vimelea vinavyoitwa Colletotrichum sp na Glomerella cingulata. 

Dalili ni madoa ya kahawia kwenye majani ambayo husambaa na kisha jani hukauka. Magonjwa haya yanaweza kudhibitiwa kwa kupiga dawa za ukungu kama Dithane M-45 kila baada ya wiki mbili.

Masoko Ya zao La Binzari

Soko la binzari linapatikana ndani na nje ya nchi pia Zao hili huuzwa katika nchi za Uganda, Kenya, Uingereza, Ujerumani, Mashariki ya Kati, n.k.

Binzari yaweza kuuzwa ikiwa mbichi (mara tu baada ya kuvuna), ikiwa kavu au baada ya kusagwa kulingana na mahitaji ya soko.

Wakulima wanashauriwa kukausha binzari kwa uangalifu ili kutoharibu ubora wake.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply