Jinsi Ya Kuwa Na Furaha Kwenye Maisha

Kufahamu jinsi ya kuwa na furaha kwenye maisha ni jambo zuri kwasababu siku zote furaha itakusaidia sana kuondokana na mawazo na kuyaona maisha ni mazuri na yenye amani.

1. Jitahidi Sana Kusamehe

Watu wengi hukosa furaha kutokana na kubeba uchungu na maumivu yaliyotokana na watu waliowakosea. Ikiwa unataka kuwa na furaha ni muhimu kumsamehe aliyekukosea hata kama hajaomba msamaha.

Kumsamehe aliyekukosea kuna manufaa kwako zaidi kuliko kwa yule aliyekukosea. Mara nyingi aliyekosea huendelea na maisha yake ya kawaida huku aliyekosewa akizidi kuumia.

2. Jitahidi Kufanya Unachokipenda

Moja kati ya siri kubwa ya kufanikiwa na kuwa na furaha katika kile unachokifanya, ni kwa kupenda kile unachokifanya.

Unapopenda kile unachokifanya, utakuwa na amani na furaha mara ukutanapo na changamoto au vikwazo.

3. Jitahidi Kuwa na Shukrani

Mara nyingi tunatazama mambo mengi kiasi cha kushindwa kuwa na shukurani kwa yale tuliyonayo. Ni rahisi kuona kuwa mambo kama vile afya, marafiki, usalama na malaz. ni mambo madogo ambayo hatupaswi kushukuru kwa ajili yake.

Kwa hakika wapo watu wanaotafuta mambo hayo lakini hawayapati Hivyo ili kupata furaha ni muhimu kutambua na kushukuru kwa yale machache tuliyonayo.

4. Jitahidi Kuwasaidia Wengine

Kumsaidia mtu mwingine siyo kumpa pesa au vitu; hata kumpa mtu ushauri au kumtia moyo kunaweza kuwa na maana kubwa kwa mtu huyo.

Unapomsaidia mtu mwingine unajisikia kuwa na thamani na furaha kwani umeweza kufanya kitu chenye manufaa kwenye maisha ya mtu mwingine.

Nakumbuka niliwahi kumshauri mtu mmoja aliyekuwa amekata tamaa kutokana na kukosa pesa baada ya muda kupita nikakutana naye, akashukuru sana kwa ushauri wangu.

Alinieleza kuwa kama siyo yale maneno niliyomweleza angekuwa ameshajiua. Ni wazi kuwa nilijihisi mwenye furaha na amani kutokana na kuweza kumsaidia mtu mwingine.

5. Jitahidi Kushirikisha Wengine

Inawezekana jambo linalokukosesha furaha kuna mtu mwingine anafahamu utatuzi wake. Hivyo kwa njia ya kumshirikisha mwingine utapata ushauri au hata utatuzi wa tatizo lako.

Jambo la kuzingatia ni kuhakikisha unamshirikisha mtu sahihi.

6. Jitahidi Kuondoa Mawazo Hasi

Mawazo gani uliyonayo kwenye fikra zako? Je unawaza tu huwezi au kushindwa? Mawazo hasi au ya kushindwa ni chanzo kikuu cha kukukosesha furaha.

Amini unaweza hatakama unaona giza; leo ni giza, kesho ni mvua lakini keshokutwa jua litawaka.

Usikate tamaa, ondoa mawazo mabaya yanayokufanya ukose furaha na mani sasa.

7. Jitahidi Kuacha Kutafuta Ukamilifu

Mara nyingi watu hukosa furaha kwa sababu wanatafuta ukamilifu. Kwa hakika hakuna binadamu aliyekamilika; wote tuna madhaifu na mapungufu ya aina mbalimbali.

Badala ya kuyatafakari madhaifu yako na kuruhusu yakukoseshe furaha; yakubali na ukabiliane nayo kwa namna bora zaidi.

8. Jitahidi Kukaa na Watu Sahihi

Je umekaa katikati ya watu wanaokulaumu, kukudharau au kukubeza kila wakati? Au pengine umekaa katikati ya watu walioshindwa wanaolaumu na kulalamikia kila kitu?

Watu wa aina hii wanakusababisha ukose furaha. Hakikisha unakaa katikati ya watu wanaokutia moyo na kukuthamini.

Epuka watu walioshindwa ambao kazi yao kubwa ni kulalamika na kulaumu kila kitu.

9. Jitahidi Kuishi Maisha Yako

Watu wengi hukosa furaha kutokana na kuishi maisha ya watu wengine. Jikubali ulivyo, usitake kuwa kama mtu mwingine kwani hutoweza na utaishia kukosa furaha.

Tambua wewe ni wa pekee na tembea katika upekee wako huo.

10. Jitahidi Sana Kujiburudisha

Je unajua kuimba? Je unapenda michezo au kusikiliza mziki? Kama jibu ni ndiyo, basi hii ni njia mojawapo amabayo inaweza kukupa furaha.

Ikiwa umekosa furaha, unaweza kuimba, kusikiliza mziki au hata kushiriki kwenye mchezo unaoupenda

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply