Jinsi Ya Kuepukana Na Hofu Kwenye Maisha

Jinsi ya kuepukana na hofu kwenye maisha ni muhimu kufahamu kwasababu hofu sio nzuri na ina madhara makubwa sana kwenye maisha yetu ya kila siku.

1. Jitahidi Kupunguza imani Potofu

Wakati mwingine watu wanapata hofu kutokana na imani au fikra potofu pekee. Kwa mfano unaogopa kinyonga kwa sababu umesikia kuwa kikikugusa utatokwa na ngozi au kufa; je una uhakika juu ya swala hili?

Maswala mengi yanayowaogopesha watu ni kutokana na imani potofu tu na wala hakuna ukweli wowote. Chunguza kama kweli swala linalokupa hofu ni la kweli au ni fikra na imani potofu tu.

2. Jitahidi Kukizoea Kile Kinachokupa Hofu

Kukikimbia kile kinachokuogopesha hakuwi suluhisho la hofu yako bali huifanya iimarike zaidi. Kwa mfano ikiwa unaogopa mbwa, basi ukimwona mbwa usikimbie; kaa na jitahidi kumzoea.

Kwa njia hii baada ya muda utaweza kukizoea kile kinachokutisha na hutokuwa na hofu tena unapokutana nacho.

3. Jitahidi Kutafakari Madhara Ya Hofu

Hebu fikiri jinsi hofu itakavyoathiri ufanisi na utendaji kazi wako; usikubali hofu ionekane kubwa kuliko madhara yake.

Kama hofu hutuzuia kufanya kazi vizuri na kwa ufanisi ule unaotakiwa, kwanini itutawale? Kwa mfano ikiwa una hofu ya mitihani umeshawahi kufikiri jinsi hofu hiyo itakavyokuathiri katika mitihani yako kuliko hata kilichokuwa kinakutisha kwenye mitihani yenyewe?

Fikiri tofauti sasa, usikubali hofu ikutawale kuliko athari zake. Ukizingatia hili hutoogopa tena hofu bali utaiepuka kwani hutokubali iathiri kile unachokifanya.

4. Jitahidi Kuacha Kuwa Mkamilifu

Kila mtu ana mapungufu yake, hivyo kuogopa kwa ajili ya udhaifu fulani au kujitahidi kuepuka hofu ili uwe mkamilifu ni makosa.

Tambua udhaifu wako na ukubali ili uweze kukabiliana nao. Epuka kuhofu mambo ambayo hayana sababu. Tambua kila mtu ana udhaifu wake; tofauti yetu ni namna tunavyokabiliana na udhaifu huo pekee.

5. Jitahidi Kukumbuka Mambo Ya furaha

Njia nynginne ya kukabiliana na hofu ni kujikumbusha mambo au maeneo ya furaha. Mara unapopatwa na hofu jikumbushe eneo au jambo ambalo huwa linakupa furaha na ujasiri.

Kumbuka, “tunavyofikiri ndivyo tunavyokuwa”. Hebu jitahidi kutafakari jinsi lile eneo au jambo lingine linavyokupa furaha na amani kuliko hata hilo dogo linalokupa hofu.

Fikiri pia jinsi ulivyokutana na mambo mengine yaliyokupa hofu kwenye maisha yako lakini yakapita bila tatizo lolote; hivyo usikubali hofu yoyote kutawala fikra zako.

6. Jitahidi Kutumia Njia za Asili

Katika kupambana na hofu, kamwe usitumie dawa au kilevi cha aina yoyote. Hofu ni swala la asili na la kisaikolojia zaidi.

Matumizi ya vitu kama pombe ili kukabiliana na hofu vinaweza kukuathiri zaidi kuliko kukusaidia.

Kwa mfano hebu fikiri unahofu ya kuzungumza mbele za watu, kisha unakunywa pombe ili upate ujasiri; moja kwa moja unaweza kufanya vituko au kuwa jasiri kupita kiasi mbele za watu na ukajiaibisha zaidi.

Kwa mfano pia, kama una hofu unapokuwa mwenyewe nyumbani, unaweza kufungua redio au televisheni ili nyumbani pasiwe kimya sana.

Ni hakika kama utazingatia njia za asili za kukabili hofu utaweza kupata matokeo mazuri zaidi.

7. Jitahidi Kuomba Ushauri

Hakuna tatizo jipya duniani; hofu inayokukabili wewe ilishawakabili watu wengi na wakafanikiwa kuishinda. Hivyo omba ushauri na zungumza na mtu sahihi ili akusaidie kukabiliana na hofu yako.

Subscription Form

Tuandikie email yako uweze kupata post za mtandao wa wauzaji kwa haraka.

Tuandikie Mawazo Yako

Leave a reply